• Nairobi
  • Last Updated March 28th, 2024 11:42 PM
Lazima Simbas iimarishe ulinzi ili kupaa – Snook

Lazima Simbas iimarishe ulinzi ili kupaa – Snook

Na Geoffrey Anene

Kocha Ian Snook amekiri Kenya Simbas ina matatizo katika idara ya ulinzi na kusema haina budi kuimarisha idara hiyo ikitaka kufuzu kushiriki Kombe la Dunia nchini Japan mwaka 2019.

Simbas haikufuzu kupitia mchujo wa Kombe la Afrika ilipomaliza nyuma ya Namibia, lakini ina nafasi ya mwisho ya kujaribu bahati itakapokabiliana na Canada, Hong Kong na Ujerumani mjini Marseille nchini Ufaransa mwezi Novemba 11-23, 2018.

Snook na vijana wake watarejelea mazoezi Septemba 3 baada ya mapumziko ya karibu majuma mawili. Walikamilisha Kombe la Afrika kwa kuzabwa na Namibia 53-28 Agosti 18 jijini Windhoek.

“Lazima tuimarishe idara ya ulinzi kabla ya kuelekea Ufaransa. Ulinzi ni mojawapo ya matatizo tulikuwa nayo katika Kombe la Afrika na lazima tuhakikishe tunarekebisha idara hii,” Snook amenukuliwa na tovuti ya KweséESPN akisema.

“Mchujo hautakuwa rahisi, lakini wachezaji wanafahamu kibarua kinachotusubiri nchini Ufaransa. Tuna uwezo wa kufuzu kushiriki Kombe la Dunia, lakini lazima tutie bidii,” aliongeza.

Raia huyu wa New Zealand ameeleza tovuti hiyo kwamba anatumai Shirikisho la Raga la Kenya (KRU) litatafutia Simbas mechi za kujipima nguvu kabla ya ziara ya Ufaransa.

Kenya, ambayo haijawahi kushiriki Kombe la Dunia la raga ya wachezaji 15 kila upande katika historia yake, itafungua mchujo huo dhidi ya Canada (Novemba 11), kisha ilimane na Hong Kong (Novemba 17) na kuukamilisha dhidi ya Ujerumani (Novemba 23).

Mshindi wa mchujo huu ataungana na New Zealand, ambao ni mabingwa watetezi, Afrika Kusini, Italia na Namibia katika Kundi B kwenye Kombe la Dunia.

Snook amejumuisha wachezaji wapya Thomas Okidia, Ephraim Oduor na Elvis Namusasi katika kikosi chake cha watu 33 na kuita tena nahodha wa zamani Wilson Kopondo, ambaye hakushiriki Kombe la Afrika. Amewatema Curtis Lilako, Oscar Simiyu, Isaac Adimo, Edmund Anya na Erick Kerre.

Kikosi cha Simbas:

Patrick Ouko, Thomas Okidia, Philip Ikambili, Dalmus Chituyi, Mohamed Omollo, Maxwell Kang’eri, Zedden Marrow, Tony Onyango (wote Homeboyz), Moses Amusala, Peter Karia, Oliver Mang’eni, Davis Chenge, Martin Owilah, Darwin Mukidza, Jacob Ojee, Peter Kilonzo (wote KCB), Ephraim Oduor, Joseph Odero, Hillary Mwanjilwa, Colman Were, Andrew Chogo, George Nyambua, Felix Ayange (wote Kabras Sugar), Samson Onsomu, Xavier Kipng’etich, Leo Seje, Vincent Mose (wote Impala Saracens), William Ambaka (Kenya Harlequin), Wilson Kopondo, Malcolm Onsando (wote Kenya Harlequin), Elkeans Musonye (Strathmore Leos), Biko Adema (Nondescripts) na Elvis Namusasi (Mombasa).

You can share this post!

Harambee Stars kupimana nguvu na Malawi Kasarani

Wasamburu waipa serikali siku 2 wamwachilie Lesiyampe

adminleo