• Nairobi
  • Last Updated April 19th, 2024 8:55 PM
Wabunge wa Jubilee waapa kumng’oa Rotich ofisini

Wabunge wa Jubilee waapa kumng’oa Rotich ofisini

Na CHARLES WANYORO

WABUNGE wawili wa chama cha Jubilee wametoa mwito kwa Rais Uhuru Kenyatta amfute kazi Waziri wa Fedha Henry Rotich wakimlaumu kwa kuchangia sera mbovu za kifedha ambazo wanasema zimedunisha hali ya uchumi.

Mbunge wa Chuka Igamba Ng’ombe, Patrick Munene na mwenzake wa Runyenjes Eric Muchangi walimlaumu Bw Rotich kutokana na hali mbaya ya kiuchumi inayoshuhudiwa, ambayo imepelekea serikali kuongeza ushuru wa VAT kwa asilimia 16 kwa bidhaa za petroli.

Wakizungumza mjini Embu, viongozi hao walishikilia kwamba watashughulikia suala hilo la VAT wakati Bunge litakapoandaa vikao maalum kesho na Alhamisi, na vile vile kuhakikisha waziri huyo anatimuliwa ofisini.

“Kabla Bunge lielekee likizoni kulikuwa na mswada wa kumtimua ofisni Bw Rotich na tutaundeleza kwa sababu hajawajibikia majukumu yake ipasavyo. Si lazima tupige kura ya kumwondoa ofisini kama waziri kwa kuwa hata yeye anajua ameshindwa na kazi. Lakini tunashindwa kwa nini amekataa kujiuzulu kwa hiari?,” akauliza Bw Munene.

Mbunge huyo alimlaumu Bw Rotich kwa kumakinikia utekelezaji wa sera za Shirika la Fedha ulimwenguni (IMF) na Benki ya Dunia kwa sababu alikuwa afisa wa zamani wa shirika hilo.

“Ukiangalia sera za kifedha anazokumbatia utaona kwamba wizara yake inaongozwa na watu waaminifu kwa shirika la IMF. Si ajabu kwamba maafisa wa ngazi za juu wa hazina hiyo walitoka shirika hilo,” akalalamika Bw Munene.

Kando na Bw Rotich aliwataja katibu wa wizara hiyo Kamau Thugge, gavana wa benki kuu Patrick Njoroge na Mkurugenzi Mkuu wa bajeti, fedha na maswala ya kiuchumi kama maafisa wa zamani wa IMF.

Bw Muchangi kwa upande wake alimtaka Bw Rotich kubeba msalaba wake kuhusiana na maswala yote ya wizara hiyo ambayo alitaja kwamba haijakuwa ikitekeleza wajibu wake vizuri.

Wakati huo huo, viongozi hao wawili vile walionya Bunge la Kitaifa dhidi ya kuandaa mkutano na kuafikia uamuzi wa kumwokoa Bw Rotich kabla ya vikao vya Jumanne na Alhamisi.

You can share this post!

Wizi wa majeneza na misalaba makaburini washangaza wakazi

Waliotoroka makwao kufuatia fujo za kisiasa waombwa kurudi

adminleo