• Nairobi
  • Last Updated April 20th, 2024 5:23 PM
TAHARIRI: Wadau watatue shida za vijana

TAHARIRI: Wadau watatue shida za vijana

NA MHARIRI

KUONGEZEKA kwa visa vya kujitoa uhai miongoni mwa vijana ni jambo ambalo linatishia msingi na mustakabali wa jamii ya sasa.

Ni suala nzito ambalo linahitaji kushughulikiwa kwa haraka, kwani mkondo huu unaendelea kupanuka kadri siku zinavyosonga.

Kulingana na takwimu ambazo zimetolewa na mashirika kadhaa ya kijamii, vijana wengi wanaojipata katika hali hii ni wale walio kati ya miaka 18 na 35.

Nayo Idara ya Polisi inasema kuwa karibu visa 1,400 vya vijana waliojitoa uhai ama waliojaribu kujitoa uhai viliripotiwa katika vituo mbalimbali vya polisi mwaka uliopita.

Tafiti kadhaa zimebaini wazi kwamba changamoto za kiuchumi, ukosefu wa ajira, matatizo ya kimapenzi ama ndoa ni baadhi ya viini vikuu vya vifo hivyo.

Ni dhahiri kwamba vijana wengi wanakabiliwa na changamoto za kiuchumi, hasa wanapobaini kwamba matumaini makubwa waliyokuwa nayo wakisoma ni kinyume na uhalisia wanaokumbana nao wanapoanza kutafuta ajira.

Wengi hutamauka wanapokumbuka juhudi nyingi walizoweka wakiwa vyuoni ama taasisi nyingine za masomo ili kufanikiwa wanapomaiza taaluma zao. Kwa haya yote, imefikia wakati ambapo lazima wadau husika wabuni sera ambayo itahakikisha kwamba kuna mpango wa kuwasaidia vijana wanaohitimu kutoka vyuo mbalimbali.

Ingawa serikali imefanya juhudi kuimarisha Hudma ya Kitaifa ya Vijana (NYS) mikakati hiyo imeonekana kutofaulu kutokana na sakata za ufisadi ambazo zimekuwa zikiripotiwa kila mara.

Hata hivyo, hilo halimaanishi kwamba juhudi hizo zinapaswa kuachwa, kwani idadi ya vijana itazidi kuongezeka.

Mfano mmoja serikali inapaswa kuiga ni kubuni hazina maalum ya kushughulikia vijana wote wanaomaliza masomo yao kama ilivyo katika nchi kama Denmark.

Chini ya mpango huo, vijana hao hupewa kiasi fulani cha pesa kujiendeleza ili kuhakikisha kwamba wanaepuka changamoto zitokanazo na ukosefu wa ajira. Kwa mfano huu, lazima Kenya iondoe hali ambapo vijana wengi huanza kulipa mikopo ya Halmashauri ya Elimu ya Juu (HELB) ilhalo wengi wao huwa hata hawana ajira.

Kwa mkakati kama huo, huenda ukawa mwanzo wa kutatua changamoto za kiuchumi ambazo zinawakumba mamilioni ya vijana nchini.

You can share this post!

Ruto aahidi wakazi fidia za ardhi

ONYANGO: EACC isijifiche kwa Biblia, iweke mikakati inayofaa

adminleo