• Nairobi
  • Last Updated April 19th, 2024 8:55 PM
Berahino kidume chumbani, afunga ‘hat trick’ kwa vichuna watatu!

Berahino kidume chumbani, afunga ‘hat trick’ kwa vichuna watatu!

Na CHRIS ADUNGO

JINA la mvamizi wa Stoke City na timu ya taifa ya Burundi, Saido Berahino lilitafunwa sana vinywani mwa wengi wiki jana baada ya kufichuka kwa habari kwamba alifunga mabao matatu ya kuhesabika kwa wanawake watatu chini ya kipindi cha wiki sita.

Sogora huyo anayedumishwa kwa mshahara wa juu zaidi kambini mwa Stoke City (Sh10 milioni kwa wiki) sasa hali wala kulala kutokana na kesi zinazomkabili mahakamani. Kulingana na gazeti la The Sun, jina la Berahino ndilo lililopo katika stakabadhi na vyeti vya kuzaliwa kwa watoto wawili waliokopolewa mnamo Mei 30 na Julai 17, 2018.

Mama wa mmoja wa watoto wa mfumaji huyo ni mchumba wake wa zamani, Stephania Christoforou ambaye alimzaa mtoto wa kiume Costa mnamo Mei 30, 2018 katika hospitali ya Birmingham Women’s, Ungereza.

Stephania alitibua ghafla mipango ya kufunga ndoa na Berahino baada ya kulifumania dume lake hilo likichovya asali katika mzinga wa mwanamitindo mzawa wa Amerika, Chelsea Lovelace katika kasri walilokuwa wakilimiki mjini Cannocks, eneo la Staffordshire, Uingereza.

Kichuna mwingine ambaye amemzalia Berahino mtoto ni demu mzawa wa Afrika mwenye umri wa miaka 28 ambaye kwa sasa anatafuta idhini ya korti ili kujumuisha jina la sogora huyo kwenye cheti cha kuzaliwa kwa mwanawe.

Mwanamke wa tatu ni Chelsea Lovelace ambaye alimzalia Berahino mtoto Aniya Marie mnamo Julai 17, 2018 katika hospitali ya Manor, eneo la Walsall, Uingereza.

Mapema Mei 2018, mama mwingine wa watoto watatu mwenye umri wa miaka 39 alikiri kwamba alikuwa akimfungulia Berahino buyu lake la asali mara kwa mara kwa kima cha Sh450,000 kwa usiku mmoja hadi kufikia mwisho wa Machi 2018.

Baada ya kuridhishwa na ufundi wa Berahino katika mechi kadhaa za faraghani walizokuwa wakichezea ‘ugenini’, mama huyo aliyekiri kuteswa na hisia za kukosa huduma za dume lake kwa muda mrefu, alianza kumtembelea Berahino nyumbani kwake Cannock. Hata hivyo, walifumaniwa na Chelsea aliyemtema mnamo Aprili 2018.

Berahino, 25, alianza kutalii mzinga wa Chelsea baada ya kuzidiwa na upweke wa kuachwa na Stephania, 27. Msingi wa uhusiano kati ya Berahino na Stephania ulianza kuyumba mnamo Novemba 2017 baada ya nyota huyo mzawa wa Burundi na raia wa Uingereza kuanza kushiriki ulevi kupindukia na kutoka kimapenzi na makahaba wa kila sampuli.

Stephania aliwahi kumsamehe Berahino mara kadhaa licha ya mazoea ya kuwaleta mahawara nyumbani kwao kisha kuponda raha nao kitandani mwake kwa malipo ya hadi Sh750,000 kwa usiku mmoja mwishoni Desemba 2017.

Berahino alichezea Burundi mchuano wake wa kwanza katika kibarua cha kufuzu kwa fainali za Kombe la Dunia (AFCON) mnamo Septemba 2018.

You can share this post!

ONYANGO: EACC isijifiche kwa Biblia, iweke mikakati inayofaa

Ujio wa Sarri na Emery unawakosesha Klopp na Guardiola...

adminleo