• Nairobi
  • Last Updated March 19th, 2024 10:15 AM
AISHA JUMWA: Ua la waridi lenye mvuto wa aina yake

AISHA JUMWA: Ua la waridi lenye mvuto wa aina yake

Na MOHAMED AHMED

MBUNGE wa Malindi, Bi Aisha Jumwa, amezidi kuibua mijadala kwenye ulingo wa kisiasa baada ya kugeuka kutoka mtetezi mkubwa wa Kiongozi wa Chama cha ODM, Bw Raila Odinga, hadi kuanza kuunga mkono azimio la Naibu Rais William Ruto ya urais mwaka wa 2022.

Bi Jumwa amekuwa kwenye mstari wa mbele miongoni mwa wabunge wa Pwani waliochaguliwa kupitia ODM ambao sasa chama hicho kinataka kuwaadhibu kwa ‘usaliti’ kwa kumuunga mkono Bw Ruto ambaye ni hasimu mkubwa wa kisiasa wa Bw Odinga.

Wakati wa kampeni za Uchaguzi Mkuu uliopita, Bi Jumwa ndiye alikuwa mwanamke ngangari ambaye angemshambulia Bw Ruto kwa mtindo wa aina yake hadi Bw Odinga akambandika jina ‘Mekatilili wa Menza’ kuashiria ujasiri wake wa uongozi wa kisiasa.? Zaidi, wengi wanamkumbuka alivyoimba, “Salama Salama Jubilee! Salama Salama! Salama Salama Bw Ruto! Mwendako muende Salama!”

Angeimba Bi Jumwa huku akifuatisha na cheche za maneno za kumkashifu Bw Ruto. Uswahiba wake na Bw Ruto ulifanya mnamo Juni, mbunge huyo akapata jina jipya la ‘Mama Rada’ wakati wa ziara ya Bw Ruto eneo la Malindi kaunti ya Kilifi kwa jinsi alivyogeuka kumkashifu Bw Odinga.

“Sisi tumekuja upande huu wa serikali kwa ajili ya manufaa ya watu wetu hivyo basi siasa za zamani za kutingisha viuno bila manufaa yoyote sisi hatuzitaki tena. Hivi viuno vina kazi yake,” akasema Bi Jumwa na kuendeleza mashambulizi dhidi ya Bw Odinga.

Katika ziara hiyo katika maeneo Kaunti hizo za Pwani Bi Jumwa alionekana kumwita majina mabaya Bw Odinga na kushutumu uongozi wa chama hicho kwa kutaka kuwachukulia hatua za kinidhamu kwa sababu ya kuungana kwao na Bw Ruto.

Lakini sasa maswali yameibuka kuhusu kama ataendeleza mtindo huu kwa muda mrefu, au hiki ni kivumbi tu ambacho kitageuza mwendo wake kulingana na jinsi upepo wa kisiasa utakavyovuma Pwani katika siku zijazo.

Kwenye mahojiano ya kipekee na Taifa Leo, Bi Jumwa alisema hana uhasama na kiongozi wake wa chama.

Alisema kuwa anamheshimu kiongozi huyo na wamekuwa wakizungumza kwa njia ya simu mara kwa mara.

“Raila bado ni kiongozi wa chama changu na nataka kusema kuwa sina uhasama na yeye. Hizi ni propaganda tu lakini tuko imara kwenye chama chetu,” akasema. Hata hivyo, wafuasi wa Bw Odinga eneo hilo wanasema mienendo ya Bi Jumwa haifai kushangaza yeyote ambaye anamfahamu kisiasa.

Mbunge wa Likoni, Bi Mishi Mboko, ambaye alikuwa rafiki wa karibu wa Bi Jumwa alisema kiongozi huyo atarudi tu chamani.

“Akiona joto limezidi, atarudi kule kule. Na sio yeye pekee bali viongozi wale wengine pia. Lakini kuondoka kwao hata hivyo hakujapunguza lolote,” akasema Bi Mboko.

Miongoni mwa viongozi wengine kutoka Pwani ambao wametangaza kumuunga mkono Bw Ruto ni pamoja na Juma Wario (Senata, Tana River), wabunge Paul Katana (Kaloleni), Ali Mbogo (Kisauni), Mohamed Ali (Nyali) Benjamin Tayari (Kinango), Michael Kingi (Magarini), Ali Wario (Garsen), Jones Mlolwa (Voi), Ali Sheriff (Lamu Mashariki), Stanley Muthama (Lamu Magharibi) Said Hiribae (Galole), Badi Twalib (Jomvu), na Mbunge Mwakilishi wa Kilifi, Getrude Mbeyu.

Hisia kwamba huenda Bi Jumwa bado ana guu moja ndani kikamilifu katika ODM unatokana pia na jinsi anapokashifu chama hicho, yeye huepuka kumshambulia Gavana wa Mombasa Hassan Joho, jinsi wafanyavyo wenzake.

Kulingana na mchanganuzi wa siasa Prof Hassan Mwakimako, Bi Jumwa amekuwa mjanja katika uasi wake dhidi ya ODM kwani anafahamu fika kwamba Bw Joho ana ushawishi zaidi katika eneo la Pwani.

Itakumbukwa kuwa Bi Jumwa anaazimia kuwania ugavana ifikapo 2022.? ? “Amekuwa akiepuka kumuandama Bw Joho kwa sababu siasa za Joho zimekita mizizi katika kanda hii, ukilanganisha na Bw Odinga ambaye ni mwanasiasa wa kitaifa.

Anajua wazi kuwa kuanzisha uhasama na Bw Joho kutaharibu siasa zake za eneo hilo kwani Joho ako na ushawishi wa karibu zaidi Pwani kuliko Bw Odinga,” akasema Prof Mwakimako.

Bw Joho amekuwa miongoni mwa viongozi wenye uwezo wa kushawishi siasa za kaunti nyingi za Pwani ikiwemo Kilifi.? ? Aidha, Prof Mwakimako aliongeza kuwa umakini wa Bi Jumwa unasababishwa na uwezekano wa kugeuka kwa wimbi la kisiasa wakati wanapoelekea mwaka 2022.

“Anajua wazi kuwa sasa bado ni mapema na siasa huenda zikabadilika na kwa sababu Bw Joho anataka kuwania kiti cha urais na hivyo basi ni lazima atambue kuwa huyo ni kiongozi wake wa kanda hiyo,” akasema.

You can share this post!

KURUNZI YA PWANI: Nyuki sasa watumiwa kupambana na mavamizi...

TAHARIRI:Tutafakari kuhusu mageuzi ya Katiba

adminleo