• Nairobi
  • Last Updated March 29th, 2024 11:05 AM
KURUNZI YA PWANI:  Tana River kujiunga na Jumuiya ya Kaunti za Pwani

KURUNZI YA PWANI: Tana River kujiunga na Jumuiya ya Kaunti za Pwani

Na STEPHEN ODUOR

KAUNTI ya Tana River itajiunga na Jumuiya ya Pwani ili kufaidi maendeleo kwa pamoja.

Gavana Dhadho Godhana alisema wikendi mjini Hola kwamba Tana River iko na nafasi nzuri ya kunawiri kiuchumi chini ya muungano wa Jumuiya ya Pwani.

“Baada ya kushauriana na viongozi wa Taifa na wenzangu katika kaunti, tulikubaliana kuwa ni vyema tukijiunga na Jumuiya ya Pwani,ambapo tutaweza afikia malengo yetu ya kiuchumi, ” alisema.

Gavana huyo alisema kuwa kaunti ya Tana River ina maazimio sawa ya kimaendeleo kama ya kaunti nyingine za Pwani.

Zaidi, alisema kuwa majimbo ya Pwani yalikuwa mfano mwema wa kuiga, kwani uchumi wao ulikuwa ukinawiri kwa kasi, jambo ambalo Tana River lilifaa kuiga kutoka kwao.

“Iwapo jimbo hili linataka kuafikia malengo yake kiuchumi, lazima ichukue hatua ya kuiga kutoka kwa wenzetu, na sisi tumekubaliana kuwa hakuna wengine wa kuiga ila wenzetu wa Pwani,” alisema.

Bw Godhana pia aliashiria kuwa iwapo kura ya maoni ingejumlisha kaunti ya Tana River pamoja na zile za Lamu na Kilifi, hakuwa na tatizo, kwani hata naye angegombea kiti cha kanda hiyo.

Alisema kuwa jimbo la Tana River halikuwa na lolote kuiga kutoka katika majimbo ya Kaskazini, kwani wote walikuwa na tatizo moja, na mbali na hilo, majimbo hayo yangeinyima jimbo hilo haki na usawa.

“Iwapo tutakuwa katika kata moja na Garissa na Wajir, hakuna cha kuiga kule kiuchumi, sote tu wagonjwa ila hapa tuna raslimali ambazo kwa hakika zitatumiwa vibaya, na pia hapatakuwa na usawa katika uongozi maana wao ni wengi kutuliko, ” alisema.

Gavana huyo alieleza kuwa Jimbo la Tana River lilikuwa katika hatua ya kujikwamua kutoka katika umasikini, na halitarudi nyuma kwa kujenga uhusiano hafifu.

Hapo awali, gavana Dhadho Godhana alikuwa amepinga hatua na juhudi za kuunganisha majimbo ya Pwani katika kutengeneza Jumuiya ya Pwani, akisema kuwa wazo hilo lilikuwa la kisiasa, na la kuwafaidi viongozi wachache waliokuwa karibu kustaafu.

You can share this post!

Bei ya mafuta taa yazidi kupanda

KURUNZI YA PWANI: Mahangaiko ya wakazi kuhusu kivuko cha...

adminleo