• Nairobi
  • Last Updated April 24th, 2024 5:50 AM
Amuua baba yake kwa kumnyima kondoo wa kulipa mahari

Amuua baba yake kwa kumnyima kondoo wa kulipa mahari

 TITUS OMINDE na STEPHEN MUNYIRI

POLISI wa eneo la Eldoret Mashariki wamemkamata mwanaume mwenye umri wa miaka 28 ambaye anashukiwa kumuua babake alipokataa kumpa kondoo wa familia ili alipe mahari kukomboa mtoto wake wa kiume aliyepata nje ya ndoa.

Polisi walisema kuwa Andrew Kimutai alimvamia baba yake akiwa chumbani mwendo wa saa moja Jumapili usiku ambapo alimkata kichwa kwa kutumia shoka.

Marehemu Joseph Marindany alifariki kutokana na majeraha kichwani alipokuwa akikimbizwa hospitalini.

Kisa hicho kilitokea wakati Kimutai alipotaka babake amruhusu auze kondoo wa familia ili alipe mahari aweze kuruhusiwa kupewa mtoto wake aliyepata nje ya ndoa na mwanamke anayeishi mjini Nakuru.

Marehemu ambaye hakujua mwanawe ana mtoto nje ya ndoa, alikataa kumpa kondoo. Mshukiwa alikasirika kabla ya kumvamia kwa shoka chumbani usiku.

Akithibitisha kisa hicho, OCPD wa Eldoret Mashariki Bw Richard Omanga alisema mshukiwa amekamatwa.

“Marehemu alikataa kumpa mwanawe kondoo kwa sababu hakujua alikuwa amezaa mtoto nje ya ndoa kama alivyodai. Mshukiwa alikasirishwa na msimamo wa babake ndiposa akamkatakata kwa shoka,” alisema OCPD Omanga.

Mshukiwa kwa sasa anazuiliwa katika kituo cha polisi cha Naiberi akisubiri kufunguliwa mashtaka baada ya uchunguzi kukamlika.

Katika mahakama ya Karatina, Kaunti ya Nyeri, mwanamume alieleza alivyopigwa na wanaume wawili kwa kukosa kulipa deni la Sh10. Bw Benson Kiprono Rotich, mfanyakazi wa shambani katika kijiji cha Itundu, Mathira Mashariki, alishangaza mahakama alipodai kwamba wanaume hao walimpiga kwa sababu hakuwa wa kabila lao.

Bw Rotich alimweleza Hakimu Elvis Michieka kuwa alienda katika hoteli mnamo Aprili 27 mwaka huu na kuagiza samosa mbili kwa bei ya Sh20 kila moja lakini baadaye aligundua hakuwa na pesa za kutosha na akamuomba mwenye hoteli amruhusu ampelekee siku iliyofuata.

Hata hivyo, alisema mwenye hoteli alikataa kumsikiliza na akamuita mfanyakazi wake na wote wawili wakaanza kumpiga kwa kipande cha mti kichwani kabla ya kuokolewa na wasamaria wema.? “Mheshimiwa, nimewafahamu vyema wawili hawa kwa muda kwa sababu ninafanya kazi karibu, mmoja alizoea kuniita mtu wa kabila tofauti lakini sikudhani ingekuwa mbaya hadi waliponishambulia.”

wakiniambia sitoki kabila lao kwa sababu ya Sh10,” alisema. Alikuwa akitoa ushahidi katika kesi ambayo Chem Kaburia na Peter Murimi wamekanusha kumpiga na kumjeruhi.

You can share this post!

Jacque Maribe na mchumba wake waanza safari ya kujinasua

Ibada ya wafu ya walioangamia ajalini kufanyika Jumatano

adminleo