• Nairobi
  • Last Updated March 28th, 2024 11:42 PM
Makamishna wapya wa IEBC wateuliwe kabla ya referenda – Opiyo Wandayi

Makamishna wapya wa IEBC wateuliwe kabla ya referenda – Opiyo Wandayi

Na CHARLES WASONGA

MBUNGE wa Ugunja Opiyo Wandayi amesisitiza kuwa sharti nafasi za makamishna wanne wa Tume Huru ya Uchaguzi na Mipaka (IEBC) zijazwe kwanza kabla ya tume hiyo kuruhusiwa kuendesha kura ya maamuzi kuhusu mabadiliko ya katiba.

Akiongea na wanahabari Jumanne katika majengo ya bunge, Nairobi mbunge alisema kuwa kura ya maamuzi “ni kibarua kikubwa ambacho hakiwezi kuendeshwa na makamishna watatu walioko sasa.”

“Kwa sababu ni wazi kuwa sharti katiba ya sasa ifanyiwe marekebisho kupitia kura ya maamuzi ningependa kamati ya bunge kuhusu haki na masuala ya sheria (JLAC) kuanza mchakato wa kubadilisha sheria ya IEBC ili kutoa nafasi ya kubuniwa kwa jopo la kuteua wamakishna wapya kuchukua mahala pa wale ambao wamajiuzulu.

Kura ya maamuzi sio uchaguzi mdogo ambao unaweza kuendeshwa na Bw Wafula Chebukati na wenzake wawili,” akasema Bw Wandayi ambaye ni ndiye mwenyekiti wa Kamati ya Bunge kuhusu Uhasibu (PAC).

Wiki jana Bw Chebukati alinukuliwa akisema kuwa kuwa tume hiyo inaweza kuendesha kura ya maaamuzi hata kabla ya nafasi za makamishna wanne waliojiondoa kujazwa.

Na siku mbili zilizopita Kamishna Boya Molu alikariri msimamo huo akinukuu kipengee cha Katiba kinachosema kuwa tume za kikatiba sharti ziwe na angalau makamishna watatu kabla ya kuruhusiiwa kuendeshwa majukumu yazo kisheria.

“Tulivyo hapa sisi ni makamishna watatu, na hivyo sisi ni kamilifu kisheria na kiutendakazi. Tunaweza kutekeleza majukumu yote kwa mujibu wa katiba, ikiwemo kura ya maamuzi, bila sheria yoyote,” akasema Bw Molu mjini Wote wakati tume hiyo ilipozindua zoezi endelevu la usajili wa wapiga kura wa wapiga kura wapya.

Makamishna ambao walijiuzulu ni; Dkt Roselyn Akombe (aliyejiondoa kabla ya marudio ya uchaguzi wa urais wa Oktoba 26, 2017) pamoja na Consolata Maina, Margaret Mwachanya na Dkt Paul Kurgar waliong’atuka Aprili 16, mwaka huu.

Wakati huo huo, Bw Wandayi na mwenyekiti wa JLAC William Cheptumo wamependekeza kuwa makamishna na wafanyakazi wote wa IEBC wachunguzwe kuhusiana na ubadhirifu wa mabilioni ya pesa za umma kuelekea uchaguzi mkuu uliopita.

Walitoa wito kwa maafisa wa Tume ya Maadili na Kupambana Ufisadi (EACC) na wenzao wa afisi ya Mkurugenzi wa Mashtaka ya Umma (DPP) waanze zoezi hilo kwa kumchunguza mwenyekiti wa tume hiyo Wafula Chebukati kwanza.

“Maafisa wa EACC, DPP na DCI hawafai kusibiri mwaliko wa Bw Chebukati kabla ya kuanza kuchunguza IEBC, wanafaa kuanza uchagunzi wa haraka kuanza kwa mwenyekiti mwenyewe, makamishna wenzake na wafanyakazi wote wa afisi kuu. Uchunguzi huo haufai kuleng Bw Ezra Chiloba pekee ambaye alifutwa kazi wiki jana,” Bw Wandayi, kauli iliyoungwa mkono na Bw Cheptumo.

“Wafanyakazi wa IEBC ambao walikuwa afisini kabla na wakati wa uchaguzi mkuu kama vile aliyekuwa Mkuregenzi wa Uchaguzi Bi Emmaculate Kassait pia hawafaio kusazwa,” akasema Bw Cheptumo ambaye ni Mbunge wa Baringo Kaskazini katika mahojiano tofauti.

Bw Wandayi alisema kamati ya PAC wakati huu inachambua ripoti ya Mhasibu Mkuu wa Serikali Edward Ouko ambayo inafichua kuwa Sh9.5 bilioni hazijulikani zilivyotumiwa na IEBC wakati wa ununuzi wa bidhaa na uagizaji wa hudumu kuelekea uchaguzi mkuu wa Agosti 8, na marudio ya uchaguzi wa urais wa Oktoba 26 mwaka 2017.

“Kama kamati tunaamini kuwa makamisha na wafanyakazi kadhaa wa IEBC walihusika katika sakata hii wala sio Chiloba pekee… ndiposa tunasema wote wanafaa kupigwa darubuni na watakaopatikana na hatia waadhibiwe kwa mujibu wa sheria,” akasisitiza.

Mnamo Jumatano, Bw Chebukati alisema kuwa amewaandikia maafisa wa EACC na DPP akiwaomba wamchunguze Bw Chiloba na maafisa wengine wanaodaiwa kufuja fedha za umma kuelekea uchaguzi mkuu uliopita.

“Nimeandikia EACC na DPP ili waanzesha uchunguzi kuhakikisha kuwa wale wote waliochangia uchaguzi mkuu uliopita kuwa ghali kupita kiasi wanashtakiwa,” mwenyekiti huyo alisema mji Wote kaunti ya Makueni alipozindua zoezi la usajili wa wapiga kura wapya.

Wiki iliyopita, IEBC ilimfuta kazi Bw Chiloba kwa kile kilichosemekana na hatua ya kukataa kufiki mbele ya kamati ya nidhamu ili ajitetee kuhusiana na madai matumizi mabaya ya fedha za wakati wa ununuzi wa vifaa vya uchaguzi.

You can share this post!

MAJI MURANG’A: Wa Iria motoni kwa kudharau kamati ya...

Akwana kusaidia kuinoa KCB ligini

adminleo