• Nairobi
  • Last Updated April 16th, 2024 6:55 PM
AKILIMALI: Wanasayansi waibuka na aina ya ndizi isiyoathiriwa na magonjwa

AKILIMALI: Wanasayansi waibuka na aina ya ndizi isiyoathiriwa na magonjwa

NA FAUSTINE NGILA

HATIMAYE wanasayansi wamepata suluhu katika juhudi zao za kusaka aina bora zaidi ya ndizi inayoweza kustahimili ugonjwa hatari wa majani kunyauka unaosababishwa na bakteria.

Ugonjwa huo, ambao husababisha ndizi kuiva bila kukomaa, kuoza na hatimaye mmea kunyauka, umeathiri pakubwa uzalishaji wa ndizi katika maeneo ya milima katika kanda ya Afrika Mashariki na kuchangia uhaba wa chakula na riziki ya mamilioni ya wakulima.

Kabla ya uvumbuzi huu, iliaminika kuwa aina zote za ndizi katika kanda hii, isipokuwa aina ya Musa balbisiana, zilikuwa zinavamiwa na ugonjwa huu wenye chimbuko lake nchini Ethiopia ambao sasa umeenea hadi Afrika ya Kati.

Kundi la watafiti lililoongozwa na mkuu wa utafiri wa ndizi katika Taasisi ya Kimataifa ya Kilimo cha Tropiki (IITA) Prof Rony Swennen, mtaalamu wa mimea Dkt George Mahuku na mwenzake Dkt Valentine Nakato walitafiti aina 72 za miche ya ndizi za familia ya Musa.

Eneo la kati la jani changa zaidi la miche ya miezi mitatu lilitiwa kioevu aina ya Xcm ambamo bakteria za ugonjwa huo husafiria.

Dalili za matokeo zilifuatiliwa kila wiki kwa miezi minne, na matokeo ya mwisho kuthibitisha kuwa Musa balbisiana ni aina ya ndizi inayostahimili bakteria hizo zinazosababisha unyaukaji wa mimea.

Hata hivyo, utafiti huu ulikuwa na changamoto zake.

Ndizi za familia ya Musa balbisiana hazivutii watafiti wengi hasa katika uzalishaji wa mbegu mpya za kimseto, kwa kuwa ni za kundi la BB, ambalo lina aina ya ndizi zenye imani ya kishirikina za Tani, ambazo miche yake yenye ndizi zinazoweza kuliwa haiwezi kukuzwa shambani kwa kuwa haipatikani na hukuzwa kwa majani yake na kutengeneza lishe ya mifugo.

Kisayansi, ndizi zinazoweza kuliwa ni za kundi la A.

Ugonjwa wa mimea ya ndizi kunyauka husababishwa na bakteria ya Xcm na dalili zake ni pamoja na majani kugeuka manjano na kunyauka, kioevu cha manjano wakati mgomba umekatwa, kudidimia kwa kichipuko cha kiume, ndizi kuiva kabla ya kukomaa, rangi tofauti ndani ya ndizi na hatimaye kufa kwa mmea mzima.

Kuenea kwake ni haraka hasa kupitia kwa vifaa vyenye bakteria hii, wadudu wanaoruka na vifaa vya kupanda na kupalilia.

Ugonjwa huu hukabiliwa na wanasayansi kwa kuufuatilia kwenye mashamba, kung’olewa kwa mimea iliyoathirika na kutia dawa vifaa vyenye maambukizo.

“Uvumbuzi huu ni muhimu sana kwa mamilioni ya wakulima wa ndizi Afrika Mashariki, kwa kuwa mbinu bora ya kuzima ugonjwa ni kuunda aina ya mimea inayoustahimili,” akasema Dkt Nakato kutoka Uganda.

Maendeleo haya basi yanawapa watafiti nafasi kutumia jeni kutokana na mmea usioathirika lakini usioliwa, kuunda aina mpya ya ndizi zinazolika, kulingana na watafiti hao.

Nchini Uganda, ndizi huchangia asilimia 20 ya kalori zote zinazotumika na kila mtu.

Xcm, bakteria sugu inayoharibu mimea ya ndizi, inapatikana katika mataifa ya Burundi, DRC, Rwanda, Tanzania, Uganda na Kenya. Kwa jumla, mataifa haya huzalisha tani milioni 21 za ndizi zenye thamani ya Sh433 bilioni, huku ugonjwa huu sasa ukitishwa kufifisha mavuno.

Katika jitihada zao za kuzalisha aina zisizoathirika na ugonjwa huo, kundi hilo la watafiti lilitumia aina zote za ndizi katika kituo chao cha IITA nchini Uganda, na kuteua aina 13, zenye uwezo wa kustahimili ugonjwa huo, unaofanana na ule wa Musa balbisiana.

Dkt Nakato aliteua seli kutokana na aina Musa acuminata, aina nyingine ya ndizi za msituni ambazo tayari imo katika mpango wa IITA wa kuzalisha ndizi za maeneo ya milimani.

Hatua hizi, alisema, zitakuwa nguzo muhimu katika mchakato wa kuzalisha miche ya ndizi zinazoliwa na zisizoathirika na ugonjwa huo.

“Matokeo ya utafiti huu ni muhimu sana kwa jamii ya kilimo cha ndizi. Kupitia matokeo haya, tutazidisha juhudi zetu za kuzalisha aina za ndizi zinazostahimili makali ya ugonjwa huo,” akasema Profesa Swennen.

Mashirika hayo mawili yanajivunia kutafiti na kuzalisha miche ya ndizi zenye mavuno ya hali ya juu ya matoke kwa jina NARITA, iliyoundwa kwa mseto wa ndizi za milimani za Afrika Mashariki na aina ya Calcutta 4, kutokana na familia ya ndizi za Musa acuminata.

Aina ya NARITA, kulingana na watafiti hao, itapimwa kama ina bakteria za unyaukaji wa mimea na huenda ikatumika kwa mipango ya siku za usoni ya kuboresha mazao ya matoke kwa kuyapa nguvu za kujikinga dhidi ya ugonjwa huo.

You can share this post!

Aliyetishia kuua msichana na kula maiti yake anaswa

AKILIMALI: Baada ya mwezi mmoja, mmea huu utakuletea faida

adminleo