• Nairobi
  • Last Updated April 23rd, 2024 8:31 PM
Mama akiona kuokota nywele katika kinyozi

Mama akiona kuokota nywele katika kinyozi

Na CORNELIUS MUTISYA

ITHAENI, MACHAKOS

Kwa Muhtasari:

  • Mwenye kinyozi aliwahudumia wateja wake na akafagia nywele. Hakujua kwamba kulikuwa na mama aliyekuwa akimtegea amalize kuzifagia.
  • Mwenye kinyozi alipoondoka, mama huyo alifika na akaanza kuziokota nywele hizo na kuzipakia kwa kikapu
  • Watu walifurika mara moja na wakaanza kumtandika mama huyo wakimtuhumu kuwa mchawi

MAMA wa umri wa makamo, alipokezwa kichapo cha mbwa koko na wakazi wa eneo hili walipofumaniwa nje ya kinyozi akiokota nywele za watu na kuzipakia katika kikapu. Wakazi walishuku alikuwa akitaka kwenda kutekeleza vituko vya ushirikina.

Kulingana na mdaku wetu, mwenye kinyozi aliwahudumia wateja wake na akafagia nywele hadi nje ili asubuhi wahudumu wa serikali ya kaunti waje kuzichukua na kuzipeleka kuzitupa kwenye jaa la takataka. Hakujua kwamba kulikuwa na mama aliyekuwa akimtegea amalize kuzifagia.

”Mhudumu wa kinyozi alifagia nywele na kuziacha nje ya mlango na akaondoka’’ akasema mdokezi.

 

Kuzitia kikapuni

Inasemekana kwamba, mwenye kinyozi alipoondoka, mama huyo alifika na akaanza kuziokota nywele hizo na kuzipakia kwa kikapu kilichochakaa. Hata hivyo, ni wakati alipokuwa akiendelea na shughuli hiyo, walinzi wawili walipomuona na wakamshuku.

Waliamua kumkabili na kumuuliza sababu ya kukusanya nywele hizo.

“Mama aliwaambia mabawabu hao alidhamiria kutengeneza gondoro na nywele hizo. Hata hivyo, jitihada zake za kujitetea ziliambulia patupu na walinzi hao wakapuliza firimbi’’ alisema mdokezi.

 

Mchawi

“Twaarifiwa kwamba, watu walifurika hapo mara moja na wakaanza kumtandika mama huyo wakimtuhumu kuwa mchawi. Alipokezwa kichapo cha mbwa koko nusura aone vimulimuli na akaokolewa na maafisa wa usalama kabla ya kutiwa moto. Wakazi walimlaumu mama huyo kwa kuwaroga akitumia nywele na vipande vya nguo zao,’’ alisema mdaku wetu.

Duru zaarifu kuwa wakazi walitaka mama huyo asukumwe seli lakini akaachiliwa kwa kukosekana kwa ushahidi wa kumhusisha na ushirikina.

 

You can share this post!

Watu wanne wafariki baada ya kukanyaga kilipuzi

OBARA: Mzaha huu wa viongozi hautamaliza majanga

adminleo