• Nairobi
  • Last Updated March 19th, 2024 6:55 AM
KURUNZI YA PWANI: Huenda wanaovamia ardhi si maskwota

KURUNZI YA PWANI: Huenda wanaovamia ardhi si maskwota

Na SAMUEL BAYA

MASWALI yameanza kuibuka kuhusu watu wanaovamia mashamba wakidai kuwa maskwota katika eneo la Pwani.

Kuna maskwota zaidi ya 10,000 ambao aidha wamevamia mashamba na kuyauza na kisha kuondoka au wanaishi katika ardhi hizo zenye mizozo katika kaunti ya Kilifi.

Baada ya kuvamia na kuharibu makao katika eneo la Kikambala wiki iliyopita, sasa polisi wanasema kuna maeneo mengine yanayolengwa ambayo yatavamiwa karibuni.

Katika mahojiano na Taifa Leo kijiji cha Mwendo wa Panya aliposimamia harakati za kuwatimua maskwota, kamanda mkuu wa polisi Kilifi, Bw Fredrick Ochieng alisema kuwa bado wanatarajia kuzuru maeneo mengine na kuwafurusha maskwota ambao wanakalia ardhi hizo.

“Huu ni mwanzo tu, bado kuna maeneo mengi ambayo watu wamevamia na kujenga makazi. Hayo pia tutayaondoa kwa sababu ardhi hizo ziko na wamiliki halali,” akasema Bw Ochieng.

Tangazo hilo la mkuu wa usalama limeleta bayana utata mwingi ambao unakabili usimamizi wa ardhi katika kaunti hiyo na Pwani kwa jumla.

Uchunguzi wa Taifa Leo umebaini kuongezeka kwa visa vya watu kuvamia mashamba ya kibinfasi kisha kujidai kuwa ni maskwota na kuanza kupambana na wamiliki halali mahakamani.

Kwa mfano uvamizi katika kijiji cha Mwendo wa Panya ulifanyika baada ya maskwota hao kupoteza kesi waliyokuwa wamewasilisha mahakamani wakidai kuwa ardhi hiyo ilikuwa ni ya kwao.

Baada ya mvutano huo wa miaka sita, mmiliki wa shamba hilo alishinda kesi na kupata kibali cha mahakama kuwaondoa.

Ardhi hiyo ni ya ekari 27 kulingana na hati za mahakama na kwa sasa kuna familia zaidi ya 800 ambazo zinaishi katika eneo hilo.

Hatua ya kuwafurusha ilisababisha uharibifu wa mali ya mamilioni ya fedha ihuku wakazi wakibaki nje bila makao.

Kulingana na Prof Halimu Shauri, tatizo la maskwota bandia limesababishwa na uchumi ambapo watu wengi huamua kuvamia mashamba na kujidai kuyamiliki.

Kisha baada ya kuvamia kwa muda mfupi huamua kuwauzia watu wengine na kuelekea eneo lingine lenye ardhi ya wazi na kuvamia tena.

“Wakazi wengi hutumia ardhi kama njia ya kujikimu. Wengi wao ni wavivu na huwa hawataki kujishughulisha na kazi za kufanya ili kupata riziki,” alisema Prof Shauri.

Aliongeza, “Mara nyingine wanapovamia mashamba haya, huwa wanatarajia kwamba serikali itawasaidia kwa kuwapatia hati za kumiliki ardhi hiyo.Kisha baadaye huuza na kuondoka na hili ni tatizo kubwa.”

Prof Shauri alisema kuwa wengi wa maskwota wanafahamu vyema historia ya mashamba katika eneo la Pwani na mara nyingi huamua kutumia sababu hizo kusema kuwa ardhi ni ya mababu zao na kuivamia.

“Hii shida ya umiliki wa mashamba ni tatizo kubwa sio tu katika eneo la Pwani ila katika taifa lote.Tunaona yale ambayo yanaendelea katika msitu wa Mau, eneo la Mlima Elgon. Changamoto ni nyingi sana na zinasabishwa na sera mbaya za ardhi ambazo zimeshinda kusimamia tatizo hili,” aliongeza.

Prof Shauri alisisitiza umuhimu wa sheria ambazo zitatua suala la ardhi nchini.

Mshirikishi wa Kenya National Land Alliance, Bw Naghib Shamsan alisema kuwa tume ya kusimamia ardhi nchini imeshindwa kufanya kazi yake ndiyo maana uvamizi wa ardhi unaendelea.

kutafuta makazi na hivyo basi kuvamia mashamba ambayo wanaona yako karibu na kuanza kujenga makazi.

“Uvamizi wa mashamba katika Kikambala na kaunti ya Kilifi kwa ujumla kumewatia hofu wawekezaji wengi kuwekeza katika maeneo hayo ya Kikambala.

Maskwota hawa wale ambao wako Kikambala, utawapata ni wale walikuwa Kwa Bulo, Mwembe Legeza na hata katika maeneo ya Kilifi,” akasema Bw Shamsan.

Afisa huyo alisema kuwa suluhisho ni kwa serikali kutoa fedha ili kuwanunulia mashamba maskwota halali na kisha waweke kwa mtandao wa serikali kuzima maskwota laghai.

“Mchezo wanaofanya maskwota hawa ni kwenda katika ardhi ya mwenyewe na kuingia dani, kisha baadaye waanze kutafuta usaidizi wa mahakama.

Baadaye mahakama huwapatia kibali cha kuendelea kuishi katika ardhi hiyo lakini wanapofurushwa, mamilioni ya fedha kupotea. Hili ni tatizo kubwa,” akasema Bw afisa huyo.

Bw Shamsan alisema kuwa tume ya NLC imefeli katika kutoa hamasisho kwa wakenya jinsi ya kufanya kuhusiana na masuala ya ardhi.

“Nilifanya utafiti wa wale ambao walikuwa wamevamia ardhi ya wenyewe katika eneo la Junda kaunti ya Mombasa na kugundua baadhi yao walikuwa wametoka katika kaunti za Kilifi, Kwale nna maeneo mengine ya eneo la Mikindani.

Tulipata kufahamu hiyo kwa sababu ya data ambayo tulichukua mwaka wa 2009,” akasema Bw Shamsan.

Aliongeza kwamba endapo NLC haitawajibika basi asilimia 100 ya uvamizi wa mashamba utaendelea.

Kaunti ya Kilifi imeshuhudia visa vingi vya uvamizi wa mashamba kuanzia katika eneo la Kibarani, Mavueni,na Kikambala.

Akiwahutubia viongozi wa mashinani katika hoteli ya Wild Waters jijini Mombasa Jumamosi iliyopita, Gavana wa Kilifi Bw Amason Kingi alisema kuwa tatizo la ardhi na uskwota ni baadhi ya dhuluma za kihistoria Wapwani wamepitia.

Viongozi hao walitarajiwa kuyaweka bayana wakati kamati ya mwafaka kati ya kiongozi wa upinzani Raila Odinga na Rais Uhuru Kenyatta ingefika Pwani. Kamati hiyo hata hivyo haikuweza kufika.

 

You can share this post!

Apewa dhamana ya Sh500,000 kwa kupokonya ajuza unga wa kilo...

TAHARIRI: Ni unafiki mkuu kumlaumu waziri kwa mimba za...

adminleo