• Nairobi
  • Last Updated April 19th, 2024 1:14 PM
Nahodha wa Simbas kukosa mechi kali dhidi ya Hong Kong

Nahodha wa Simbas kukosa mechi kali dhidi ya Hong Kong

Na GEOFFREY ANENE

NAHODHA Davis Chenge atakosa mechi ya Kenya Simbas ya kufa kupona dhidi ya Hong Kong ya kufuzu kushiriki Kombe la Dunia la raga ya wachezaji 15 kila upande mjini Marseille, Ufaransa hapo Novemba 17, 2019.

Chenge, ambaye ni mchezaji wa klabu ya KCB jijini Nairobi, aliumia bega katika mechi ya ufunguzi ya mchujo huu wa mataifa manne dhidi ya Canada mnamo Novemba 11. Simbas iliumizwa kwa alama 65-19 katika mechi hiyo.

Kocha Ian Snook amefanya mabadiliko sita katika kikosi kilichopoteza dhidi ya Canada akilenga kutafuta ushindi wa kufufua kampeni ya Kenya.

Amempa nahodha wa zamani Wilson K’opondo majukumu ya unahodha. Pia ataanzisha K’Opondo pamoja na Elkeans Musonye, Felix Ayange na Nelson Oyoo katika mechi hii. Nao Ephraim Oduor na Dalmus Chituyi wataingia kama wachezaji wa akiba.

Mohammed Omollo, Moses Amusala, Oliver Mang’eni na Darwin Mukidza wamepumzishwa wikendi hii. Benchi la kiufundi linatarajia Chenge kuwa fiti kushiriki mechi ya mwisho dhidi ya Ujerumani hapo Novemba 23. Kutoka orodha hii ya mataifa manne, timu itakayokamilisha juu ya jedwali itaingia Kombe la Dunia litakalofanyika nchini Japan mwaka 2019. Itamenyana na New Zealand, Afrika Kusini, Italia na Namibia katika Kundi B.

Kikosi cha Simbas kitakachovaana na Hong Kong: Wachezaji 15 wa kwanza – Patrick Ouko, Colman Were, Joseph Odero, Wilson K’opondo (nahodha), Malcolm Onsando, Andrew Amonde, Elkeans Musonye, Joshua Chisanga, Felix Ayange, Samuel Oliech, William Ambaka, Leo Seje Owade, Collins Injera, Nelson Oyoo na Tony Onyango;

Wachezaji wa akiba – Philip Ikambili, Ephraim Oduor, Hilary Mwanjilwa, George Nyambua, Martin Owilah, Samson Onsomu, William Reeve na Dalmus Chituyi.

Historia kati ya Kenya na Hong Kong

Desemba 13, 2011: Hong Kong 44-17 Kenya (Dubai, Cup of Nations)

Agosti 23, 2016: Kenya 24-18 Hong Kong (Nairobi, Kirafiki)

Agosti 26, 2016: Kenya 34-10 Hong Kong (Nairobi, Kirafiki)

Agosti 20, 2017: Kenya 19-19 Hong Kong (Nairobi, Kirafiki)

Agosti 26, 2017: Kenya 34-43 Hong Kong (Nairobi, Kirafiki)

Novemba 18, 2017: Hong Kong 40-30 Kenya (Hong Kong, Cup of Nations)

You can share this post!

Safaricom yawafaa wanawake wajawazito

Sayari mpya yapatikana karibu na jua

adminleo