• Nairobi
  • Last Updated April 19th, 2024 8:55 PM
AKILIMALI: Jinsi ya kufanikisha ufugaji wa ng’ombe wa maziwa

AKILIMALI: Jinsi ya kufanikisha ufugaji wa ng’ombe wa maziwa

Na PETER CHANGTOEK

ILI kufanikiwa katika kilimo cha ufugaji wa ng’ombe wanaofugwa kwa ajili ya maziwa, ni jambo aula kufahamu fika kwamba, lishe bora ni muhimu mno.

Kufanikiwa kuzaa kwa ng’ombe kwa njia iliyo salama ni mojawapo ya mambo muhimu katika kilimo cha ufugaji wa ng’ombe wa maziwa.

Kuzaa kwa njia salama kwa ng’ombe kunachangia kuzalishwa kwa maziwa kwa wingi. Hili litawezekana tu, iwapo ng’ombe aliyezaa ndama atatunzwa vyema, kabla, wakati wa kuzaa, na baada ya kuzaa,’’ asema Wytze Heida, mtaalamu wa masuala ya mifugo ambaye pia ni mkurugenzi wa shirika la SNV.

Mtaalamu huyo anasema kuwa, ng’ombe anapozaa, hupitia mabadiliko za kila aina, yakiwemo mabadiliko ya mwilini, kisaikolojia, na kadhalika, na hivyo basi kiwango cha lishe ambazo anafaa kulishwa vilevile, kinafaa kubadilishwa, kuambatana na mahitaji ya ng’ombe.

Bw Heida anafichua kuwa, kwa wakati huo, ng’ombe aliyezaa anastahili kulishwa kwa lishe zinazompa nguvu mwilini, ambazo pia zitamfanya kuyazalisha maziwa kwa wingi.

Wataalamu kutoka Chuo Kikuu cha Minnesota, nao wanasema kwamba, zipo awamu tatu ambazo zinaweza kutumika kuwalisha ng’ombe wa maziwa, ili kuhakikisha kuwa wanayazalisha maziwa kwa wingi, na kuwa na afya.

Awamu ya kwanza ni wakati ng’ombe anapozaa hadi siku ya sabini baada ya kuzaa. Kwa wakati huo, maziwa huongezeka upesi mno, hususan katika wiki ya sita hadi ya nane, baada ya kuzaa. Nafaka wanazolishwa ng’ombe wa maziwa kwa muda huo, zinafaa kuongezwaongezwa kidogo kidogo kila siku. Hata hivyo, mkulima ajihadhari asije akawalisha kwa nafaka nyingi kupindukia, kwa sababu zitaathiri afya yao.

Pia, wataalamu hao wanasema kwamba, nafaka nyingi zinazokithiri kiasi kinachofaa, zitaathiri kiwango cha mafuta yaliyoko kwa maziwa. Katika awamu iyo hiyo, lishe zenye nyuzinyuzi zitumike kwa kiasi fulani, kuwalisha.

Isitoshe, lishe zenye protini zitumike kuwalisha ng’ombe hao. Kiwango cha protini chategemea mambo kadha wa kadha, mathalan mbinu za kulisha, uwezo wa uzalishaji wa maziwa kwa ng’ombe, miongoni mwa mambo mengineyo.

Hali kadhalika, mkulima anafaa kuwalisha kwa lishe bora ambazo ni za kiwango cha juu. Vilevile, lishe ziwe na virutubisho vyote vinavyotakikana. Aidha, mkulima ahakikishe kuwa ng’ombe wake hawaathiriwi na usumbufu wa akili, maadamu jambo hilo huathiri kiwango cha maziwa yanayozalishwa.

Awamu ya pili ni kuanzia siku ya sabini hadi siku ya mia moja na arobaini. Huo ni wakati ambapo maziwa yanaanza kupungua. Hivyo basi, ni jambo aula kutumia mbinu zote kuzuia hali hiyo ya kupungua kwa maziwa.

Kwa wakati huo, ng’ombe hawafai kuupunguza uzani, bali wanafaa kuushikilia uzani walionao, au kuuongeza. Kwa hivyo, walishwe kwa lishe zifaazo. Hata hivyo, zisizidi kiasi kinachofaa. Katika awamu hiyo hiyo, ng’ombe hawafai kuwa na mambo yanayowatatiza akili.

Katika awamu ya tatu ya ulishaji wa ng’ombe, ambayo huanzia siku ya 140 hadi siku ya 305, kiwango cha maziwa huwa kinapungua, na ng’ombe anafaa kuwa na mimba.

You can share this post!

AKILIMALI: Kijana aungama anautambua utamu wa mapapai

AKILIMALI: Saladi isiyolikuzwa na wengi ingawa ina soko tamu

adminleo