• Nairobi
  • Last Updated April 23rd, 2024 10:10 AM
2019: Mgomo kuanza Alhamisi huku Knut ikikaza kamba

2019: Mgomo kuanza Alhamisi huku Knut ikikaza kamba

Na CHARLES WASONGA

NI rasmi sasa kwamba shughuli za masomo katika shule zote za umma nchini zitatatizika kuanzia Alhamisi wiki hii shule zitakapofunguliwa kwa muhula wa kwanza mwaka huu.

Hii ni baada Katibu Mkuu wa Chama cha Walimu Nchini (Knut) Wilson Sossion kushikilia kuwa mgomo huo utaendelea ulivyopangwa baada mkutano wa kupatanisha chama hicho na Tume ya Kuajiri Walimu (TSC) kufeli kughulikia malalamishi manne makuu ya walimu.

Kwenye barua kwa wenyeviti na waweka hazina wa matawi yote ya Knut nchini, Bw Sossion jana aliwataka viongozi hao kuhakikisha kuwa mgomo huo unaanza siku ya kwanza ya kufunguliwa kwa shule.

“Barua hii inalenga kujulisha kila mwanachama kwamba mgomo unaanza tarehe ya kwanza ya muhula wa kwanza. Walimu wote wasiripoti shuleni kwa muhula wa kwanza hadi mgomo utakapofutiliwa mbali rasmi na Katibu Mkuu kupitia uamuzi wa Baraza Kuu la Kitaifa (NEC) kwa mujibu wa Katiba yetu,” Bw Sossion akasema.

Akaongeza: “Tafadhali wafahamisheni walimu wote katika matawi yenu yote kuhusu mgomo huu kwa sababu ni wajibu wao kuungana kupigania masihali yao kama walimu wa taifa hili.”

Bw Sossion alitaja uhamisho wa walimu, kandarasi ya utendakazi, kupandishwa vyeo kwa walimu na mafunzo ya ziada ya walimu kama masuala makuu ambayo Knut inataka TSC ishughulikie kwa njia “itakayowaridhisha walimu” ndiposa walikubali kufutilia mbali mgomo.

Knut inaitaka TSC kufutilia mbali uhamisho wa zaidi ya walimu wakuu 3,000 iliutekeleza mwanzoni mwa mwezi jana pamoja na kuwapandisha vyeo walimu 30,000. Vile vile, walimu wanataka kusitishwa kwa sera ya utathmini wa utendakazi wa walimu ulioanza kutekelezwa mwaka jana na walimu wapewa nafasi ya kujiongeza kimasomo.

“Hatutarejea kazini hadi pale masuala haya yote yatakapotatuliwa. Tunawaomba walimu wote kushiriki mgomo huu wa kihistoria kama njia ya kutetea haki yetu,” akasisitiza Bw Sossion huku akishikilia kuwa mgomo huo ni halali kisheria na kikatiba.

Mnamo Jumamosi mkutano kati ya Knut na kamati ya upatanisho iliyobuniwa na Wizara ya Leba ilifeli kuzaa matunda.

Baada na mkutano huo ulioandaliwa katika makao makuu wa Knut, Nairobi, Bw Sossion alisema kuwa maelewano yalikosa kuafikiwa kwa sababu ya “ukosefu wa nia njema kutoka kwa TSC”.

“Kwa sababu TSC ilishikilia mpango wake wa awali wa kutekeleza uhamisho wa walimu, mwafaka hautapatikana,” akasema Bw Sossion ambaye pia ni Mbunge Maalum wa chama cha ODM.

Leo maafisa wa Wizara ya Leba, wakiongozwa na Waziri Ukur Yattani wanapangiwa kufanya mkutano mwingine na viongozi wa Knut katika jaribio la kuzuia mgomo huo ambao utawaathiri zaidi ya wanafunzi milioni nne. Hata hivyo, kufikia jana jioni kufanyika kwa mkutano huo hakukuwa kumethibitishwa.

Iwapo mgomo huo utafanyika, utawatatiza wazazi na wanafunzi ambao wamekuwa wakifanya maandalizi ya kuanza kwa muhula wa kwanza kuanzia Januari 3. Wanafunzi wa kidato cha kwanza wanaotarajiwa kuripoti shuleni kuanzia Januari 7 pia wataathirika.

You can share this post!

LSK kufika kortini ikitaka DCI akome kukamata washukiwa...

Wakulima washtuka Rais hajapata ripoti ya mahindi

adminleo