• Nairobi
  • Last Updated April 25th, 2024 7:45 AM
Madaktari huiba dawa za wagonjwa Migori na kuziuza TZ – Polisi

Madaktari huiba dawa za wagonjwa Migori na kuziuza TZ – Polisi

Na VIVERE NANDIEMO

MADAKTARI na walinzi katika hospitali za Kaunti ya Migori huenda wanashirikiana kuiba vifaa na dawa na kuviuza nchi jirani ya Tanzania.

Haya yalifichuka juzi baada ya polisi mjini Migori kumkamata mlinzi akiwa na vifaa vya hospitali ya rufaa ya kaunti hiyo.

Taifa Leo iligundua kwamba maafisa katika hospitali hiyo wameunda njama ya kuiba dawa na vifaa na polisi wanashuku kwamba baadhi ya maafisa wakuu, matabibu na walinzi wanahusika.

Vifaa vinavyoibwa huuziwa kliniki za kibinafsi mjini Migori na vingine katika nchi jirani ya Tanzania. Inasemekana kuwa baadhi ya madaktari wanamiliki kliniki ambazo huwa wanatumia dawa wanazoiba kutoka hospitali za umma.

Mwaka jana, Gavana Okoth Obado, alilalamika kuwa dawa na vifaa katika hospitali za umma huuzwa nchiniTanzania.

Wagonjwa katika hospitali hizo wamekuwa wakilalamikia ukosefu wa dawa huku wakitumwa kuzinunua nje ya hospitali.

“Hospitali hii ni aibu kubwa. Kila wakati mtu anaambiwa akanunue dawa kwa sababu haina dawa. Hali hii imekuwa kwa muda,” alisema mkazi wa mji wa Migori.

Mnamo Jumanne, polisi walimkamata mlinzi anayeshukiwa kuwa mmoja wa wanaotumiwa kuiba dawa na vifaa kutoka hospitali ya rufaa ya Migori.

Maafisa wa polisi waliopashwa habari na umma walipata vifaa hivyo na dawa za thamani ya Sh4 milioni.

Maafisa hao walimfuata mlinzi huyo hadi katika nyumba yake na kumkamata.

“Tulipata habari kutoka kwa umma na polisi wakamfuata mlinzi hadi nyumbani kwake katika mtaa wa Oruba mjini Migori ambapo walipata vifaa hivyo,” alisema mkuu wa polisi (OCPD) Patrick Macharia.

Miongoni mwa vifaa vilivyopatikana ni mashini ya eksirei, vifaa vya kutumiwa katika chumba cha upasuaji, kompyuta na runinga.

“Mlinzi huyo atashtakiwa baada ya uchunguzi kukamilika,” alisema Bw Macharia.

Maafisa wakuu wa hospitali ya rufaa ya Migori walikiri kwamba vifaa hivyo vilikuwa mali ya hospitali hiyo.

You can share this post!

Wasichana wa Narok kuchunguzwa kama wamekeketwa

Oliech arejea KPL, Gor kumlipa Sh350,000 kwa mwezi

adminleo