• Nairobi
  • Last Updated April 20th, 2024 9:55 AM
TAHARIRI: Wabunge waache kutumiwa visivyo

TAHARIRI: Wabunge waache kutumiwa visivyo

Bw Rashid Achesa aliyeidhinishwa na  wabunge kusimamia Wizara ya Michezo. Picha/Maktaba

Na MHARIRI

Kifupi:

  • Ni muhimu wabunge watathmini kwa kina uwezo wa baadhi ya walioteuliwa na kuzingatia masuala nyeti yaliyoibuliwa
  • Wabunge wa Jubilee waweke maslahi ya chama kando, na kuhakikisha wamewapa Wakenya mawaziri wanaofaa
  • Kuna Wakenya wengi wanaohitimu kuongoza wizara  kwa hivyo haifai kwa Rais kuteua wasiofaa kwa sababu za kisiasa
  • Dkt Matiang’i alifanya kazi mufti katika sekta ya elimu na ni vyema wabunge wapate sababu kwa nini alihamishwa

BAADA ya kuwapiga msasa watu waliopendekezwa na Rais Uhuru Kenyatta kuhudumu katika Baraza la Mawaziri, wabunge jana walianza kuijadili ripoti kuhusu shughuli hiyo.

Tayari kuna utata kuhusu kiwango cha masomo cha baadhi ya walioteuliwa, na ni muhimu wabunge watathmini kwa kina uwezo wa baadhi ya walioteuliwa na kuzingatia masuala nyeti yaliyoibuliwa na umma kuwahusu.

Kwa mara nyingine, inasikitisha kuwa wabunge wa upinzani walisusia kikao cha kujadili ripoti hiyo Jumatano na kuachia wabunge wa chama tawala cha Jubilee nafasi ya wazi kuidhinisha majina hayo.

Ni muhimu wabunge husika wa Jubilee waweke maslahi ya chama chao kando, na kuhakikisha wamewapa Wakenya mawaziri wanaofaa kuwahudumia kikamilifu, bila kujiingiza katika masuala ya siasa.

Wito wetu ni kwa wabunge husika wasisite kutowaidhinisha baadhi ya walioteuliwa iwapo kuna ushahidi wa kutosha kuwa hawataweza kuchapa kazi ipasavyo.

Alipotangaza Baraza la Mawaziri, Rais Kenyatta alisema anaendelea kuunda serikali yake, na kwa hivyo kuna nafasi ya kufanya mabadiliko.

Kauli hiyo inatoa fursa kwa Wakenya kumpa Rais Kenyatta rai zao, kuhusiana na baadhi ya watu aliowapendekeza.

Mmoja wa walioteuliwa alieleza wabunge wazi kuwa elimu yake iliishia shule ya msingi na ni muhimu kudumisha hadhi ya afisi ya waziri wa serikali kwa kuhakikisha kuwa anafuzu kuongoza wataalamu wengine katika wizara yake.

Kando na utata wa kiwango cha masomo miongoni mwa baadhi ya walioteuliwa, kumeibuka tashwishi kuhusiana na kuhamishwa kwa Dkt Fred Matiang’i kutoka Wizara ya Elimu hadi ile ya Usalama.

 

Sababu ya Matiang’i kuhamishwa

Ni wazi Dkt Matiang’i alifanya kazi mufti katika sekta ya elimu na ni vyema wabunge wapate sababu nzuri kutoka kwa rais kwa nini waziri huyu ahamishwe hadi wizara ya usalama.

Sharti wabunge watathmini masuala kama haya kwa kina kabla ya kuwaidhinisha waliopendekezwa.

Kuna Wakenya wengi wanaohitimu kuongoza wizara na idara mbalimbali za serikali kwa hivyo haifai kwa Rais kushinikiza kuteua wasiofaa kwa sababu za kisiasa.

Itakuwa jambo la busara kwa rais kuhakikisha hatamu yake ya mwisho uongozi haijakumbwa na msukosuko kutokana na uzembe na ufisadi kwa kuwateua watu wenye maadili na waliohitimu.

You can share this post!

Wakenya wafukuza donge nono Diamond League, wakwepa Jumuiya...

WANDERI: Valentino ni hadaa ya usasa inayodunisha tamaduni...

adminleo