• Nairobi
  • Last Updated April 18th, 2024 9:55 AM
Chama cha Jubilee chasimama na ‘Baba’

Chama cha Jubilee chasimama na ‘Baba’

CHARLES WASONGA Na WANDERI KAMAU

CHAMA cha Jubilee Jumatano kilijitokeza kumtetea kiongozi wa ODM, Raila Odinga dhidi ya shutuma za baadhi ya viongozi kuwa ndiye kiini cha mizozo inayokikumba kwa sasa.

Katibu Mkuu Raphael Tuju alitetea muafaka wa maridhiano kati ya Rais Uhuru Kenyatta na kiongozi wa upinzani Raila Odinga akisema unaafikiana azma ya Jubilee ya kuunganisha Wakenya wote na kamwe hahusiki katika mzozo wa chama hicho.

“Azma ya chama chetu, ambayo imekuwa ikikaririwa na Rais Kenyatta kila mara ni kuunganisha Wakenya wote bila kujali misingi yao ya kidini, rangi, kabila au vyama vya kisiasa. Ni moyo huu ambao ulimwongoza Rais kuweka muafaka kati yake na waziri mkuu wa zamani Raila Odinga,” akasema Bw Tuju.

Chama cha Jubilee kimekumbwa na mizozo ya ndani kutokana na suala la urithi, huku baadhi ya wakuu wake wakisisitiza Naibu Rais William Ruto hatapewa tiketi ya moja kwa moja kuwania urais 2022, nao wafuasi wake wakiitisha uchaguzi na mageuzi ya chama.

Bw Tuju alisema mzozo unaokumba Jubilee unatokana na wanachama ambao wanaongozwa na siasa za kikabila na hawataki kukubali ukweli wa mwafaka kati ya Rais Kenyatta na Bw Odinga.

Kauli hiyo iliungwa mkono na viongozi wa eneo la Mlima Kenya wakiongozwa na waliokuwa wabunge Peter Kenneth na Martha Karua, ambao walimsifu Bw Odinga na Rais Kenyatta kwa kuweka tofauti zao kando kwa ajili ya amani na umoja wa taifa.

“Ni maoni yetu kuwa baadhi ya wanasiasa wasio na uzalendo wana nia ya kuvuruga juhudi za maridhiano ili kujinufaisha binafsi kisiasa,” akasema Bw Kenneth kwenye taarifa.

Wanasiasa wanaoegemea kilichokuwa chama cha URP kabla ya kuingia Jubilee, wamekuwa wakilalamika kuwa Bw Odinga anatumia mwafaka wake na Rais Kenyatta kuingia kwenye serikali na kuvuruga umoja wa Jubilee.

Tangu mwafaka huo, Rais ameonekana kuwa na urafiki wa karibu na Bw Odinga na wamekuwa wakiandamana kwenye hafla nyingi za kiserikali na za kibinafsi, huku akimwita “ndugu yangu” kwenye hotuba zake.

Suala hilo limeonekana kuwakera baadhi ya wanasiasa wa Jubilee ambao wanaonelea kuwa rais anaegemea zaidi kwa Bw Odinga, ambaye alikuwa adui yake mkuu kisiasa kwenye uchaguzi wa 2017, na kumtenga naibu wake William Ruto.

Mbunge wa Bahati, Kimani Ngunjiri mnamo wikendi alimshutumu rais akisema amesahau mchango wa Bw Ruto katika kampeni zake za urais 2013 na 2017.

Mzozo huo pia umechochewa na maoni kuwa Bw Odinga anataka kuvunja chama hicho tawala kwa lengo la kujiweka katika nafasi bora ya kushinda urais 2022. Lakini Bw Odinga amekuwa akikanusha madai hayo.

Baadhi ya wakosoaji wake wanasema historia yake ya kuvuruga vyama na miungano ambayo amekuwa nayo awali ndiyo inayowatia wasiwasi kuwa nia yake ni kusambaratisha Jubilee.

Mzozo wa sasa ulipamba moto kufuatia matamshi ya aliyekuwa naibu mwenyekiti wa Jubilee, David Murathe kwamba hakukuwa na maafikiano kuwa Bw Ruto atakuwa mgombea urais kwa tiketi ya Jubilee 2022.

Matamshi ya Bw Murathe yalisababisha cheche ndani ya Jubilee huku baadhi ya viongozi wa chama hicho wakiongozwa na Gavana wa Kirinyaga, Anne Waiguru wakitaka yeye na Bw Tuju watimuliwe na maafisa wapya wachaguliwe. Bw Murathe alijiuzulu wiki jana.

Mzozo huo wa Jubilee unatishia kufanikiwa kwa Ajenda Nne Kuu za Maendeleo pamoja na uboreshaji wa maisha ya Wakenya kutokana na migawanyiko ambayo imeibuka serikalini.

Katika maeneo mbambali ya nchi kumeibuka kambi ambapo moja inaegemea upande wa Bw Ruto maarufu kama “Team Tanga Tanga” na nyingine inayompinga. Maeneo ambako kambi hizi zimeshamiri ni Mlima Kenya, Magharibi na Pwani.

Migawanyiko hii hasa miongoni mwa wabunge, imepatia siasa kipa umbele kuliko maendeleo, hali ambayo imezima matumaini ya wananchi kutimiziwa ahadi ambazo waliahidiwa kwenye uchaguzi wa 2017.

Eneo la Mlima Kenya ndilo limeonekana kutatizwa zaidi na siasa za 2022 huku viongozi wakigawanyika na kutumia muda wao mwingi kwenye siasa.

You can share this post!

Watu wasahaulifu sana wana akili nyingi – Utafiti

Serikali kukopa zaidi mwaka huu

adminleo