• Nairobi
  • Last Updated April 24th, 2024 10:08 PM
Wazee wapuuza madai ya vurugu Jubilee isiposimama na Ruto

Wazee wapuuza madai ya vurugu Jubilee isiposimama na Ruto

Na FRANCIS MUREITHI

BARAZA la Wazee wa Jamii ya Wakalenjin katika Kaunti ya Nakuru , limepuuzilia mbali madai ya vurugu iwapo Naibu wa Rais William Ruto, hataungwa mkono na chama cha Jubilee katika kinyang’anyiro cha urais 2022.

“Kaunti ya Nakuru itaendelea kuwa na amani hata kama Naibu wa Rais atakosa tiketi ya Jubilee kuwania urais katika uchaguzi mkuu ujao. Madai kwamba kutakuwa na vurugu hayana msingi na ni porojo zinazolenga kuzua hali ya taharuki,” akasema Mshirikishi wa Baraza la Wakalenjin, Bw Andrew Yatich.

Wakati huo huo, katibu wa chama cha ODM tawi la Nakuru, Bw Hilton Abiola alimshtumu mbunge wa Bahati, Bw Kimani Ngunjiri huku akimtaka amheshimu Rais Uhuru Kenyatta na kiongozi wa Upinzani Raila Odinga.

Bw Yatich ambaye ni msimamizi wa masuala ya amani katika baraza hilo, alisema jamii hiyo haifai kuhusishwa na kauli hiyo ya kuchochea vurugu.

“Wazee wa jamii ya Wakalenjin hatuna mawazo hayo potovu kuhusu kuzua vurugu ikiwa Dkt Ruto atanyimwa tiketi ya Jubilee 2022 kuwania urais. Hakutakuwa na machafuko Nakuru,” akasema Bw Yatich. Wazee wa baraza hilo waliitaka serikali kukabiliana na wanasiasa wanaoongoza vijana kufanya maandamano dhidi ya Rais Kenyatta mjini Nakuru.

“Rais ni nembo ya umoja wa kitaifa na wanasiasa kama mbunge wa Bahati Kimani Ngunjiri ambao wameonyesha ukaidi wanafaa kukabiliwa vikali,” akasema Bw Yatich.

Wazee wa Jamii ya Wakalenjin pia walishutumu baadhi ya wanasiasa kutoka eneo la Mlima Kenya wanaodai kuwa wametelekezwa na Rais Kenyatta katika miradi ya maendeleo.

“Rais anaitakia nchi hii mema, si kura za Mlima Kenya pekee zilizomfanya Rais Kenyatta kuingia mamlkani. Alipata kura kutoka kila eneo la nchi hii na aliapa kuwatumikia Wakenya wote bila ubaguzi,” akasema Bw Yatich.

Alisema matamshi hayo ya Bw Ngunjiri yanalenga kuzua hali ya taharuki haswa katika maeneo ya Nakuru.

“Wanasiasa wanafaa kukumbatia na mpango wa R ais Kenyatta na Bw Odinga wa kutaka kuunganisha Wakenya wote na kuzika tofauti za kikabila zisiozkuwa na manufaa kwa Wakenya,” akasema.

You can share this post!

Msongamano wa wanafunzi waathiri elimu ya chekechea

Ushauri wa Gathoni wa Muchomba kuhusu 2022

adminleo