• Nairobi
  • Last Updated April 23rd, 2024 12:34 PM
Polisi lawamani kwa kumcharaza na kumjeruhi mwanamke

Polisi lawamani kwa kumcharaza na kumjeruhi mwanamke

NA KALUME KAZUNGU

MAAFISA wa polisi Kaunti ya Lamu wamemulikwa kwa mara nyingine kufuatia kisa cha kumpiga mwanamke na kumuumiza raia kaunti ya Lamu.

Bi Mariam Wanjiru ambaye ni mkazi wa kijiji cha Manda, anadai haki baada ya kupigwa na kuumizwa na polisi wakati akitoka dukani kununua bidhaa.

Bi Wanjiru,43, ambaye alikuwa ameandamana na watoto wake watatu, anadai kucharazwa na polisi hao wanaodaiwa kumwangusha chini, hivyo kumsababishia majeraha ya shingo na mashavu.

Bi Wanjiru anaendelea kupokea matibabu kwenye hospitali kuu ya King Fahad mjini Lamu.

Aidha juhudi za mwathiriwa kutafuta fomu ya matibabu (P3) kutoka kituo cha polisi cha Lamu zimegonga mwamba kwani polisi wanadaiwa kumnyima fomu hiyo.

“Nilikuwa nimetoka dukani kununua bidhaa. Ilikuwa yapata saa mbili usiku. Nilikuwa nimeandamana na watoto wangu. Ghafla polisi wanne walitujia na kuanza kunipiga na kuniangusha chini. Waliniumiza shingo yangu na mashavu na tayari nimetibiwa hapa hospitalini King Fahad. Nimejaribu kutafuta P3 kituoni lakinio kila ninapofika ninazungushwa. Ninahitaji msaada ili nipate haki,” akasema Bi Wanjiru.

Dadake Mwathiriwa, Bi Miriam Njeri, al;iambia Taifa Leo kwamba visa vya polisi kuwap[iga na kuwaumiza ovyo wakazi eneo la Manda vimekithiri mno.

Bi Njeri aliwaomba wakuu wa usalama Kaunti ya Lamu kuwachunguza wadogo zao kwa kuendeleza ukiukaji wa haki za binadamu kila wanapokuwa kazini.

“Polisi wafaa kutulinda badala ya kutuumiza siosi raia. Dadangu tayari ni mgonjwa wa moyo na tangu tukio hilo lijiri, hali yake ya kawaida haijarejea,” akasema Bi Njeri.

Hiki ni kisa cha pili cha polisi kuwapiga na kuwajeruhi raia katika kipindi cha wiki mbili zilizopita, kaunti ya Lamu.

Wiki jana, familia moja ilijitokeza kudai haki kwa kijana wao aliyepigwa na kuumizwa vibaya na poliosi eneo la Ndau, Kaunti Ndogo ya Lamu Mashariki.

Bw Yusuf Abuu,19, alipigwa na kuumizwa matumbo yake, hatua ambayo ilipelekea yeye kufanyiwa upasuaji wa nyongo yake kwenye hospitali hiyo ya King Fahad.

Juhudi za kumpata Kamanda wa Polisi wa Kaunmti ya Lamu ili kuzungumzia suala hilo ziligonga mwamba kwani hakupokea simu.

You can share this post!

Mtoto wa miaka 13 ashangaza kuunda kampuni ya programu za...

Wakazi waandamana wakitaka kampuni ya mawe ifungwe

adminleo