• Nairobi
  • Last Updated March 29th, 2024 11:05 AM
Kenya yapoteza watalii 2,000 wakihofia usalama

Kenya yapoteza watalii 2,000 wakihofia usalama

Na Winnie Atieno

KENYA imepoteza watalii 2,000 wa kimataifa baada ya meli mbili za kifahari, zilizokuwa zitie nan’ga katika Bandari ya Mombasa, kubadilisha mkondo na kuelekea nchi nyingine.

Meli hizo ambazo huleta raia wa Ulaya kuzuru mbuga za wanyama nchini Kenya zilibadilisha mkondo kufuatia onyo la Amerika kwamba kutakuwa na shambulio la kigaidi.

Waziri wa Utalii, Najib Balala alielezea ghadhabu yake kufuatia hatua hiyo.

“Nitawasiliana na wizara ya mambo ya kigeni kuhusiana na suala hili. Onyo la Amerika limeleta taharuki na hata meli mbili za watalii kubadilisha mkondo.”

Akiongea kwenye warsha na wabunge katika hoteli ya Whitesands huko Mombasa, Bw Balala alisema meli hizo zingeleta Zaidi ya wageni 2000.

Bw Balala alisema onyo hilo litapelekea kuharibika kwa biashara za wakneya na uchumi wa taifa.

Alisema baada ya shambulizi la kigaidi huko Nairobi katika mkahawa wa DusitD2 mnamo Januari 15, alikutana na mabalozi wa nchi za kigeni ikiwemo ile ya Marekani na wakakubaliana dhidi ya kutoa onyo la usafiri kwa raia wao.

“Tulikubaliana kuwa ugaidi si swala la nchi hii bali jinamizi la ulimwengu, lazima tushirikiane. . Onyo la Marekani kwa raia wake linanuia kuwataka wawe waangalifu na makini kufuatia tishio la shambulizi la kigaidi,” Bw Balala alisisitiza.

Waziri huyo alisema vikosi vya usalama nchini vimeimarisha usalama kwa watalii na raia wake huku akisisitiza kuwa kuna usalama wa kutosha.

Aliwataka mabalozi kushirikiana na serikali kabla ya kutoa onyo la usafiri.

“Msifanya kuwe na wasiwasi, Kenya iko salama na tumekabiliana na tishio lolote,” Bw Balala alisisitiza.

Jumapili meli ya watalii ya, MS Nautica ambayo ilinuiwa kutia nang’a katika bandari ya Mombasa ilielekea Ushelisheli kufuatia onyo la Marekani.

Sekta ya utalii ilipata pigo kubwa kufuatia onyo hilo.

You can share this post!

Mbegu mbovu zasababisha uhaba wa viazi nchini

Mke aliyeenda kuokoa ndoa kwa mganga alishwa talaka

adminleo