• Nairobi
  • Last Updated April 25th, 2024 4:25 PM
Polo asukumiwa makonde mazito kwa kunyima mama hela za saluni

Polo asukumiwa makonde mazito kwa kunyima mama hela za saluni

Na CORNELIUS MUTISYA

KAVIANI, MACHAKOS

KIOJA kilishuhudiwa eneo hili mama wa umri wa makamo alipomsukumia mumewe makonde mazitomazito alipomnyima hela za kwenda saluni kusukwa.

Kulingana na mdaku wetu, polo aliuza parachichi kwa mawakala na alipotia kibindoni hela, akili ilimruka na akafululiza moja kwa moja kwa mama pima kujienjoi.

“Hakika, maskini akipata, matako hulia mbwata. Polo alipouza avakado, alijitoma baa kujienjoi na kusahamu majukumu yake mengine,’’ alisema mdokezi.

Twaarifiwa kwamba, polo alikuwa ameuza matunda hayo baada ya kuafikiana na mama watoto kuwa angemkabidhi hela zote ili aende saluni kusukwa, kugharimia vipodozi vyake na kununua chakula. Hata hivyo alighairi nia alipopata hela hizo.

Na alipokuwa akibugia mvinyo, mama watoto alijitoma ndani ya baa akiwa amepandwa na hasira za mkizi na akamparamia. Alimwaga pombe yote iliyokuwa mezani na akaanza kumfokea kwa hamaki.

“Umeuza avakado ili uje kulewa? Nipe hela za saluni haraka!’’ mama alimfokea mumewe.

Inasemekana kwamba, rabsha ilizuka ndani ya baa na mama watoto akamtwanga mumewe makonde mazitomazito nusura aone vimulimuli. “ Jamaa alikuwa amelewa kiasi cha kutojikinga dhidi ya kipigo cha mkewe,” alieleza mdokezi.

Hata hivyo, walevi waliingilia kati na kuwatenganisha wawili hao. Walimhimiza polo ampe mama watoto hela zilizobaki ili aende saluni kama walivyokuwa wamekubaliana wakiwa kwao nyumbani.

“Polo alimkabidhi mkewe pesa zilizobaki na hali ikawa shwari,” alisema mdaku wetu.
Mama alimuonya mumewe akome kumchezea kisha akaenda zake saluni na akaawacha walevi wakiendelea kupiga mtindi.

 

You can share this post!

TAHARIRI: Umma usitwikwe mzigo wa madeni

Jeshi latoa ahadi ya kusajili wanawake zaidi siku zijazo

adminleo