• Nairobi
  • Last Updated April 20th, 2024 12:46 PM
Tobiko aanza kazi kwa kuonya wafanyabiashara haramu wakatao miti

Tobiko aanza kazi kwa kuonya wafanyabiashara haramu wakatao miti

Waziri mpya wa Mazingira na Misitu, Keriako Tobiko. Picha/ Maktaba

Na LEONARD ONYANGO

WAZIRI wa Mazingira na Misitu Keriako Tobiko ameapa kukabiliana na wafanyabiashara laghai wanaokata miti ovyo bila kibali.

Bw Tobiko, aliyekuwa akizungumza mara baada ya kutwaa rasmi wizara kutoka kwa Bi Judi Wakhungu, alionya kuwa maafisa wa wizara wanaoshirikiana na wafanyabiashara hao laghai watatimuliwa na kushtakiwa.

Waziri Tobiko alisema lengo lake kuu ni kuhakikisha kuwa asilimia 10 ya ardhi ya Kenya inakuwa na miti, kulingana na katiba.

“Nimekuwa nikisoma katika vyombo vya habari kwamba maafisa wa serikali wanashirikiana na wafanyabiashara laghai kukata miti ovyo kinyume cha sheria. Ninawaonya kuwa wahusika wote watakamatwa na kushtakiwa bila kujali urafiki wao na viongozi wa juu serikalini,” akasema Bw Tobiko.

Alionya kuwa wafanyabiashara waliopewa kibali cha kukata miti watapokonywa leseni hizo iwapo watapatikana wakikiuka sheria.
Waziri alitoa onyo hilo huku idadi ya malori yanayosafirisha mbao kutoka Mlima Kenya na misitu ya Aberdare na mistu mingineyo yakizidi kuongezeka.

Hali hiyo imewatia hofu wanaharakati wa kutunza mazingira hasa kutoka maeneo ya Mlima Kenya kuhofia kwamba wakataji miti haramu wamepenyeza katika misitu hiyo ambayo ni vyanzo vya maji.

“Sheria inahitaji kuwa unapokata mti unapanda mwingine, lakini wao wanakata bila kupanda. Wafanyabiashara wa aina hiyo watapokonywa leseni na kukabiliwa kisheria,” akasema.

Bw Tobiko alisema kuwa marufuku dhidi ya matumizi ya mifuko ya plastiki itaendelea.

“Juhudi za watu wanaopinga marufuku ya mifuko ya plastiki kutaka marufuku kuondolewa haitafua dafu,” akasema Bw Tobiko.

 

You can share this post!

Chanzo cha uskwota Pwani ni unyakuzi wa ardhi – Ripoti

Hali ya hatari nchini Ethiopia kudumu kwa miezi sita ijayo

adminleo