• Nairobi
  • Last Updated April 25th, 2024 7:45 AM
DINI: Kujipenda binafsi ni mtihani, mtu anaweza kuwa adui wa nafsi yake

DINI: Kujipenda binafsi ni mtihani, mtu anaweza kuwa adui wa nafsi yake

NA PADRE FAUSTIN KAMUGISHA

Kujipenda si ubinafsi, kujipenda si uchoyo, kujipenda si kujipendelea maana huwezi kumpenda mtu kama hujipendi. Kujipenda ni kujikubali, kujithamini na kujitambua.

Ushahidi kuwa watu wengi hawajipendi umejaa kama hewa. Mtu anaweka vikombe vizuri vya chai kwa ajili ya wageni yeye kila mara anatumia vikombe vilivyopasuka na vyenye mwanya, jambo hilo ni ushahidi wa kutojipenda.

Fundi seremala hana kiti kizuri cha kukalia wakati anawatengenezea wengine viti vizuri, jambo hilo ni ushahidi wa kutojipenda. Kumbuka adui wa mtu ni mtu. Unaweza kuwa adui wa nafsi yako.

Kuna baba fulani alienda shambani na kamba kwa ajili ya kujinyonga. Mtoto wake baada ya kushinda bahati nasibu ya milioni hamsini alimtafuta baba yake kumpa habari njema. Aliambiwa ameenda shambani. Alipofika shambani alimkuta anajiandaa kujinyonga. Alimwambia habari njema ya ushindi na kuongeza kuwa kama ameamua kufanya hivyo angepewa mazishi mazuri maana pesa ipo.

Baba huyo alimwambia mtoto wake, “Acha upumbavu, njoo ukate kamba hii twende tusherekehe ufufuko wangu.” Kitendo alichotaka kukifanya Baba huyo alikuwa hajipendi, lakini huenda alikuwa ni mgonjwa kisaikolojia.

Kushughulika sana na kutokustahili kwako ni kutojipenda. Unastahili kujipenda. Kama unawajali wengine si jambo baya kujijali. Swali ni namna gani ujipende?

Kwanza, kuwa mwema kwako na kwa wengine. Una ushauri mzuri unaowapa wengine na wewe uweke katika matendo. Tuna wajibu wa kuwa wema. Muombe Mungu aikamilishe kazi njema aliyoianza. “Yeye aliyeianza kazi yake njema mioyoni mwenu, ataiendeleza na kuikamilisha” (Wafilipi 1:6).

Pili, jitunze, “Kujitunza si tendo la ubinafsi – ni utunzaji wa zawadi pekee niliyo nayo, zawadi ambayo niliwekwa dunia kuitoa kwa wengine,” alisema Parker Palmer. Utakavyokuwa ni zawadi yako kwa wengine.

Tatu, usijihukumu, “Ilinichukua muda mrefu kutojihukumu kupitia macho ya mtu mwingine,” alisema Sally Field. Acha kujilinganisha na wengine. “Umekuwa ukijisema vibaya kwa miaka mingi, haikufanya kazi. Jaribu kujikubali na uone litakalotokea,” alisema Louise L. Hay. Sema maneno mazuri juu yako. Nne, fikiria mafanikio yako na sikushindwa kwako. “Kuanzisha jambo la kujiheshimu kweli lazima kuwa makini kwenye mafanikio yetu na kusahau juu ya kushindwa na hasi katika maisha yetu,” alisema Denis Waitley.

Tano, jithamini. “Kama hujithamini, hutathamini muda wako. Na kama hutathamini muda wako, hutafanya lolote na muda wako,” alisema M. Scott Peck. Sita, jiamini.

“Kwa nini tuogope watu wanachofikiria juu yetu, je tuna imani zaidi na maoni yao kuliko maoni yetu? Alihoji Brigham Young. Saba, jua kilichoko ndani mwako ni kikubwa. “kilichoko nyuma yako na kilichoko mbele yako ni mambo madogo ukilinganisha kilichomo ndani mwako,” alisema Ralph Waldo Emerson.

Nane, jitawale na jithibiti. Tawala hisia zako, tawala, ulimi wako, tawala mawazo yako hutakuwa na mjukuu anayeitwa majuto. Kukumbuka wewe ni mtu binafsi. “kumbuka kuwa kila mara kuwa hauna tu haki ya kuwa mtu binafsi bali una wajibu wa kuwa mtu binafsi,” alisema Eleanor Roosevelt.

Tisa, usiogope. Fanya zuri unaloliogopa kufanya. Mungu yuko pamoja nawe. “Basi, usiogope, mimi nipo pamoja nawe. Usifadhaike, mimi ni Mungu wako. Nitakuimarisha na kukusaidia; nitakulinda kwa mkono wangu wa ushindi (Isaya 41:10).

Kumi, amua kuwa maisha yako ni maisha yako. “Siku nzuri sana ya maisha yako ni siku ambayo unaamua kuwa maisha yako ni yako. Hakuna kuomba msamaha au visingizio, hakuna wa kuegemea, kutegemea au kulaumu. Zawadi ni yako – ni safari ya kustaajabisha – na wewe peke yako unawajibika kwa ubora wake. Hii ni siku ambayo maisha yako yanaanza kweli,” alisema Bob Moawad.

You can share this post!

KINAYA: Msage kabisa ‘Hustler’ la sivyo akusage...

Atorokea kwa wakwe kuhepa kipigo cha mke

adminleo