• Nairobi
  • Last Updated April 16th, 2024 6:55 PM
Sitaki mimba tena, asema mama aliyejifungua watoto 5

Sitaki mimba tena, asema mama aliyejifungua watoto 5

 SHABAN MAKOKHA na CHARLES WASONGA

MWANAMKE mwenye umri wa miaka 28 amejifungua watoto watano kwa mpigo, katika Hospitali ya Rufaa ya Kakamega.

Bi Everline Namukhula kutoka kijiji cha Shisokhe, kaunti ndogo ya Navakholo alijifungua pacha watano- wavulana wawili na wasichana watatu- mnamo Jumanne usiku kupitia upasuaji.

“Nafurai na natoa shukrani kwa Mungu kwa kunipa watoto hawa watano. Sasa nina jumla ya watoto tisa. Nina wengine wanne na kifungua mimba wangu mwenye umri wa miaka 10 yuko katika darasa la pili,” akasema Bi Nakukhula.

Mumewe ni kiziwi na hufanya kazi za vibarua kijijini humo. Bi Namukhula alisema hataki kupata watoto zaidi kwani huenda akashindwa kubeba gharama ya kuwatunza.

Alisema alipoanza kuhisi uchungu wa kuzaa alienda moja kwa moja hadi katika hospitali ya kaunti ndogo ya Navakholo ambako amekuwa akihudumiwa akitaraji kujifungua mwanawe wa tano.

Watoto watano waliozaliwa, kwa mpigo, katika Hospitali ya Rufaa ya Kakamega na Bi Everline Namukhula. Picha/ Shabaan Makokha

“Baada ya kuchunguzwa niliambiwa kuwa nilikuwa nimewabeba watoto watatu. Sikutarajia kujifungua watoto watano. Kwa sasa naomba nisipate mimba tena,” akasema alipoongea na wanahabari kitandani mwake katika kitengo cha kujifungua kina mama.

Alihamishwa hadi Hospitali hiyo ya Rufaa ilipobainika kuwa alikuwa amewabeba zaidi ya watoto watatu.

Dkt Githinji Ndung’u mmoja wa madaktari waliosaidia kujifungua, alisema walimpokea hospitali humo, kutoka hospitali ya kaunti ndogo ya Navakholo, mnamo Jumanne.

“Tulilazimishwa kumsaidia kujifungua kupitia upasuaji mwendo wa saa mbili usiku,” akasema Dkt Githinji.

Waziri wa Afya katika kaunti ya Kakamega Rachael Okumu aliahidi kuisajili familia hiyo katika Hazina ya Kitaifa ya Bima ya Matibabu (NHIF) na kuwalipia ada kwa muda wa mwaka mmoja.

You can share this post!

HILLARY MUTYAMBAI: Tajriba pana ya ujasusi

Mwanamke Kakamega ajifungua pacha watano kwa mpigo

adminleo