• Nairobi
  • Last Updated April 24th, 2024 10:08 PM
AKILIMALI: Mkulima chipukizi wa ndizi anayevuma Rongai

AKILIMALI: Mkulima chipukizi wa ndizi anayevuma Rongai

Na FRANCIS MUREITHI

HUKU akiwa amevalia shati la samawati lenye mikono mifupi, kofia ya samawati na suruali ndefu ya rangi sawia, na viatu vya raba chapa gumboots, Patrick Kigen yuko kwenye shamba lake la ndizi katika eneo la Ol Rongai, kaunti ya Nakuru.

Hata bila ya kuinua kichwa chake juu Kigen ambaye ndio mwanzo umri wake unagonga miaka 28, anafyeka magugu na kuondosha matawi yaliyokauka kwenye ndizi wakati Akilimali ilipomtembelea hivi majuzi.

Mkulima huyu chipukizi amepanda migomba ya ndizi kwa shamba robo ekari na uchu wa ukulima wa ndizi aliupata kutoka kwa mamake Jane Tuigong ambaye alivuma zama zake kama mkulima shupavu wa ndizi katika eneo hili ambalo linapakana na mlima Menengai.

“Nilikuwa nafurahia kula ndizi tamu ambazo zilivunwa moja kwa moja kutoka shambani na mama mzazi. Hili lilinipa motisha kuwa hata na mimi siku moja nitabobea na kuwa mkulima mahiri wa ndizi,” anasema Kigen ambaye ni mtaalamu wa ulimwengu wa teknolojia ya taarifa na mawasiliano.

Na ili kufaulu katika kilimo cha upanzi wa ndizi aina ya FHIA 17, Grand naine na Williams, Kigen huchimba shimo la urefu wa kati ya futi moja unusu na futi mbili na upana sawia na huo.

Aidha anadokeza kuwa wakati mkulima anachimba shimo hilo ni sharti ahakikishe mchanga unaotoa kutoka juu ya ardhi na ule unaopatikana ndani ya shimo hauchanganywi.

“Miche ya ndizi yapaswa kutengana kwa kati ya mita tatu hadi mita nne ili kuipa miche hiyo nafasi ya kumea vizuri na kupata jua la kutosha. Kisha, mkulima anahitajika kuweka ndani ya shimo mbolea iliyokolea na kisha kuchanganya na mchanga mwororo alioutoa ndani ya shimo. Kisha kinachofuata ni kupanda miche na kuacha kibakuli cha maji na kuweka matawi yaliyokauka juu kuzuia unyevu na maji kuyeyuka wakati wa kiangazi,” anaelezea Kigen.

Ubora

Mbali na kuzuia unyevu na maji kuyeyuka, maganda yaliyokauka husaidia pakubwa kuchangia kuimarisha kiwango cha ubora wa udongo kwa kuzuia kukua kwa magugu haribifu.

Ili kuzuia magonjwa na wadudu waharibifu, kama vile konokono na magonjwa mengine kama vile fusarium, yeye hunyunyuzia mimea yake dawa.

Ukulima wa ndizi una gharama zake hasa wakati wa kuanza kilimo hiki kwa vile mimea hushambuliwa na wadudu hatari ambao husababisha ugonjwa wa kupooza na ikiwa mkulima hatanyunyuzia madawa mapema huenda akapata hasara kubwa,” anasema Kigen.

Kigen huvuna kati ya mikungu mitano hadi 10 ya ndizi kila wiki na kisha kuiuza kati ya Sh200 na Sh800 kulingana na uzito na urefu wa mkungu.

“Wakati kilimo kimenawiri mimi huweka kibindoni kati ya Sh5,000 na sh10,000 kila wiki wakati nawasilisha ndizi zangu sokoni,” anasema Kigen.

Afisa wa kilimo cha matunda katika Kaunti ya Nakuru Joseph Gaturuku anasema kuwa ili wakulima wa ndizi wanufaike na jasho lao ni sharti wahakikishe wanafanyia udongo uchunguzi ili kubaini kama una magonjwa na endapo watafanya hivyo huenda wakapata mavuno kemkem.

“Uchunguzi wa udongo ni muhimu sana katika kilimo cha ndizi kwa vile mmea wa ndizi huchukua muda mrefu shambani na ni kupitia uchunguzi wa udongo ambapo mkulima atafahamu magonjwa yanayoweza kukwaza kilimo chake,” anasema Gaturuku.

Anatoa mwito kwa wakulima kumwagilia mimea yao maji kwa wingi.

You can share this post!

AKILIMALI: Ufugaji wa batamzinga, kanga na batabukini wampa...

AKILIMALI: Ugumu wa kazi EPZ ulimpa wazo la biashara ya...

adminleo