• Nairobi
  • Last Updated April 24th, 2024 8:12 PM
MAWAIDHA YA KIISLAMU: Wafahamu baadhi ya Salaf wenye utukufu

MAWAIDHA YA KIISLAMU: Wafahamu baadhi ya Salaf wenye utukufu

Na HAWA ALI

SIFA zote njema anastahiki Mwenyezi Mungu, Muumba wa mbingu na ardhi na vilivyomo.

Swala na salamu zimwendee Mtume Muhammad Swallallahu ‘Alayhi Wasallam, Maswahaba zake kiram na watangu wema hadi siku ya Kiyaamah.

Daraja ya Maswahaba na heshima yao katika Dini ni jambo lisilokubali kujadiliwa na Mwislamu yeyote mkweli mwenye kupenda haki, kwa sababu hawa ndio ambao Mwenyezi Mungu Aliwahusisha kwa kuwafanya kuwa sahibu zake Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llaahu ‘alayhi wa sallam), wakamsadiki na kumfuata na kumnusuru na wakaifuata nuru aliyokuja nayo, na wakafanya kila juhudi kwa kujitolea roho zao na mali zao kwa ajili ya kuipigania Dini hii tukufu mpaka ilipokamilika.

Hawa ndio wale waliosifiwa na Mwenyezi Mungu walipoambiwa kuwa wao ni umma bora kupita zote zilizoletwa kwa ajili ya watu. Na Mwenyezi Mungu Akaridhika nao.

Tutawabainisha baadhi yao leo.

Abu Dharr al-Ghifaariy (Radhiya Allaahu ‘Anhu)

Abu Dharr al-Ghifaariy Jundub bin Junaadah bin Sakn alikuwa ni miongoni waliosimu mwanzoni lakini alichelewa kufanya Hijrah hivyo hakushiriki vita vya Badr. Fadhila zake ni nyingi na alikufa mwaka 32H.

‘Abdullaah bin ‘Abbaas (Radhiya Allaahu ‘Anhu)

‘Abdullaah bin ‘Abbaas bin ‘Abdul-Muttwalib bin Haashim bin ‘Abd Manaaf al-Qurashiy al-Haashimiy, alikuwa ni binamu yake Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) na alikuwa mfasiri wa Qur’an. Alizaliwa miaka mitatu baada ya Hijrah na alikuwa anaitwa ‘Bahari ya Elimu.’ Alikufa mwaka 68H.

‘Abdullaah bin ‘Amr (Radhiya Allaahu ‘Anhu)

‘Abdullaah bin ‘Amr bin al-’Aasw bin Waail bin Haashim bin Su’ayd bin Sa’d bin Sahm as-Sahmi. Yeye na baba yake walikuwa ni Maswahaba. Alikuwa anajua kusoma na kuandika na alipata ruhusa kutoka kwa Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) ya kuandika yote yale aliyokuwa akiyazungumza Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam). Alikufa katika mwaka 65H.

‘Abdullaah bin Mas’uwd (Radhiya Allaahu ‘Anhu)

Alikuwa Swahaba mkubwa wa Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam),‘alikufa katika mwaka 32H huko Madiynah. Az-Zubayr aliongoza Swalah ya Janaazah lake na kuzikwa Baqiy’.

Alikuwa ni mtu wa sita kusilimu hata kabla ya ‘Umar bin al-Khattwaab (Radhiya Allaahu ‘Anhu). Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) alimbashiria makazi yake Peponi. ‘Aliy (Radhiya Allaahu ‘Anhu) alitaja jambo hili kusema ya kwamba Mtume alimuamuru Ibn Mas’uwd kupanda mti kuchuma kitu fulani na kuleta chini. Maswahaba walikuwa wakiangalia miundi ya Ibn Mas’uwd wakati akipanda mti na waliaanza kumcheka kutokana na uwembamba wa miundi yake.

Mjumbe wa Allaah alisema: “Ni kitu gani kinachowachekesha? Miguu ya Ibn Mas’uwd ni mizito kwenye mizani siku ya Qiyaamah kuliko Mlima Uhud.”
[Imesimuliwa na Imaam Ahmad katika Musnad yake na kuthibitishwa na Shaykh Ahmad Shaakir (920)].
‘Abdullaah bin Mas’uwd alikuwa msomaji mkubwa wa Kurani Tukufu. Inasemekana alikuwa ni mmoja wa watu wenye kufuata kwa karibu sana mwongozo wa Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam).

Abu ad-Dardaa (Radhiya Allaahu ‘Ahnu)

Abu ad-Dardaa Uwaymir bin Maalik bin Zayd bin Qays al-Khazrajiy al-Answaariy. Kuna maoni tofauti kuhusu jina lake. Alisilimu wakati wa vita vya Badr na alishuhudia vita vya Uhud. Alikuwa ni Mwanachuoni wa Shari’ah. Mchaji Allaah miongoni mwa Swahaba. Alikufa katika mwaka 32H.

Abu Hurayrah (Radhiya Allaahu ‘Anhu)

Abu Hurayrah, ‘Abdur-Rahmaan bin Swakhr ad-Dawsiy alikwenda kwa Mtume kama Muhaajir wakati wa vita vya Khaybar. Alihifadhi idadi kubwa ya Hadiyth. Zaidi ya Hadiyth elfu nane zilisimuliwa kutoka kwake. Alikufa katika mwaka 58H.
Mtume Alimuombea du’aa yeye na mama yake kwa kusema: “Ee Allaah! Wajaalie hawa waja wako (wawili) ni wenye kupendwa na Waumini na wafanye Waumini ni wenye kuwapenda.” [Imesimuliwa na Muslim].

Abu Muwsaa al-Asha’riy (Radhiya Allaahu ‘Anhu)

Abu Muwsaa al-Ash’ariy ‘Abdullah bin Qays bin Saalim alikuwa ni mwenye sauti nzuri wakati wa kusoma Qur-aan na ni mmoja wa Wanachuoni miongoni mwa Maswahaba. Inasemekana alikufa mwaka wa 42H au 44H.

Abu Sa’iyd al-Khudriy (Radhiya Allaahu ‘Anhu)

Abu Sa’iyd al-Khudriy Sa’ad bin Maalik bin Sinaan bin ‘Ubayd al-Answaariy al-Khazrajiy. Yeye na baba yake wote walikuwa ni Maswahaba na alishuhudia vita vyote vilivyofuata baada ya vita vya Uhud. Alikuwa ni mmojawapo wa Wanachuoni miongoni mwa Maswahaba na alisimulia Hadiyth nyingi za Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam). Alikufa katika mwaka 74H.

‘Adiy Bin Haatim (Radhiya Allaahu ‘Anhu)

‘Adiy bin Haatim bin ‘Abdillaah bin Saa’d bin al-Hashraj bin ‘Aamr al-Qays at-Twaaiy, Abu Tarif. Alikuwa Mkristo aliyesilimu na kuhudhuria vita vya Jamal, Swiffiyn na an-Nahrawaan pamoja na ‘Aliy. Alikufa katika mwaka 68H.

Al-Mughiyrah Bin Shu’bah (Radhiya Allaahu ‘Anhu)

Al-Mughiyrah bin Shu’bah bin Abi ‘Aamir bin Mas’uwd ath-Thaqafiy, Abu ‘Abdillaah. Alihudhuria vita vya Hudaybiyyah, Al-Yamaamah na alipata ushindi kule Syria na Iraq. Alikufa katika mwaka 50H.

‘Amr Bin al-‘Aasw (Radhiya Allaahu ‘Anhu)

‘Amr bin al-’Aasw bin Wa’il al-Qurashiy as-Sahmiy Alisilimu katika mwaka wa Sulhu Hudaybiyyah na alikuwa ni mmoja wapo kati ya wale walioshinda kule Misr. Alifariki katika mwaka 43H.

Anas Bin Maalik (Radhiya Allaahu ‘Anhu)

Anas bin Maalik bin an-Nadr, Abu Hamzah, al-Answaariy, an-Najjaariy. Alikuwa mfanyakazi wa Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam). ambaye alikaa naye karibu kwa takriban miaka kumi tangu alipohama mpaka kifo cha Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam). Alikuwa ni miongoni mwa Maswahaba wa mwisho kufariki. Alifariki kule Baswrah akiwa na miaka 103.
Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam). Alimuombea du’aa kwa kusema: “Ee Allaah Mjalie utajiri na watoto na Vibariki vile ulivyomruzuku.” [Muslim].
Na katika mapokezi mengine Anas Aliongezea kwa kusema: “Na (kutoka kwa) Allaah fungu langu limekuwa kubwa watoto wangu na wajukuu wameongezeka kiasi cha kufikia mia moja kwa kuwahesabu.” [Muslim].

You can share this post!

TAHARIRI: Ripoti ya ukaguzi Makueni yatia moyo

OLE NDIYE! Ni rasmi sasa mikoba ya United ni ya Gunnar

adminleo