• Nairobi
  • Last Updated March 29th, 2024 7:50 AM
MAPOZI: Dr King’ori

MAPOZI: Dr King’ori

Na PAULINE ONGAJI

IWAPO wewe ni mraibu wa vipindi vya televisheni, basi huenda u shabiki mkuu wa The Wicked Edition, kipindi kinachopeperushwa na kituo cha runinga cha NTV na ambacho mhusika mkuu ni Dr King’ori.

Kazi yake safi imemwezesha kushiriki katika baadhi ya vipindi maarufu vya ucheshi nchini ikiwa ni pamoja na Kenya Kona, Offside Show na hata Churchill Show, na katika harakati hizo kujiundia jina kama mmojawapo wa wacheshi wanaotambulika na kuheshimika nchini.

The Wicked Edition kinachotambulika kutokana na kuangazia masuala halisi kwa kutumia tashtiti kimelinganishwa na kile cha Daily Show, chake mcheshi Trevor Noah.

Lakini ni ucheshi wake ambao mara kwa mara unaakisi utafiti wa kina kuhusu masuala yanayokabili nchi uliomvumisha, kumjengea himaya ya mashabiki na kuweka jina lake kwenye ramani ya wacheshi wa kutajika.

Ufanisi wake umemfanya pia kutambulika na vigogo katika ulimwengu wa burudani na utangazaji nchini Kenya, kama vile mcheshi Kazungu Matano maarufu Captain Otoyo, na mtangazaji Larry Madowo.

Mzawa wa eneo la Blue Valley, Kaunti ya Embu, Dr King’ori alianza kuonyesha kipaji chake cha ucheshi akiwa angali mdogo ambapo akiwa katika darasa la tatu, tayari alikuwa ashabandikwa jina ‘Makokha’, lake mcheshi maarufu aliyetamba kupitia kipindi cha Vioja Mahakamani.

Wanafunzi wenzake kila mara wangemteua kila mnenaji au chale alipohitajika.

Cha kushangaza ni kwamba wakati huo hakuwa na ujasiri kuhusu uwezo wake ambapo kila alipovumbua kichekesho, angemweleza mwenzake ili akiwasilishe kwa wenzake darasani.

Kadhalika alikuwa akiwatangazia wenzake kuwa wakati mmoja atakuwa na shoo yake kwenye televisheni, ndoto ambayo wengi waliipuza.

Hata hivyo ujasiri na kujiamini kwake kulimwezesha kupiga msasa kipaji chake hasa kupitia uigizaji wake wa riwaya shuleni baada ya kukamilisha shule ya upili.

Baadaye alisafiri hadi jijini Nairobi na kutembelea jumba la Nation Centre kuwasilisha wazo la shoo yake.

Mwanzoni haikuwa rahisi kwani hata baada ya kupewa fursa ya kubuni jaribio la kipindi, alikumbana na changamoto ya pesa za kufadhili mradi huu.

Lakini hakufa moyo ambapo baadaye alibahatika rafiki yake alipompa ofa ya kuandika mswada wa ucheshi katika shindano la GBS.

Kazi yake safi ilimhifadhia mwaliko wa yeye pia kushiriki huku akiwa mmojawapo wa washindi.

Na ni hapa ndipo safari yake kama mcheshi wa kulipwa iling’oa nanga. Huo ulikuwa mwaka wa 2010, wakati ambao pia aligundua anaweza kujipatia kipato kwa kuchekesha watu.

Wakati huu alikuwa akitumbuiza hasa katika klabu, kabla ya kuanza kuchangia katika kipindi cha Kenya Kona ambapo alifanya kazi kwa mwaka mmoja.

Kazi yasifika

Akiwa hapa, kazi yake ilisifika sana hata miongoni mwa watu mashuhuri katika fani hii. Mmoja wao alikuwa mcheshi Kazungu Matano ambaye alifurahishwa na jinsi alivyokuwa akipanga ucheshi wake.

Mwaka wa 2013 alimuomba aandikie kipindi cha Offside Show katika kituo cha televisheni cha NTV ambapo pamoja waliunda vipindi 69 huku akiunda kitambulisho chake kama Kinyanjui.

Kinachomtenganisha na wacheshi wengine wa kawaida humu nchini ni uthabiti wake katika kutafiti na kuhusisha masuala muhimu katika ucheshi wake.

Anasema mambo bado na ndoto yake ni kuvunja kabisa mipaka ya ukabila nchini akitumia ucheshi na pia kuteka ulingo wa kimataifa karibuni.


You can share this post!

Barclays yaamriwa ilipe serikali magari iliyonunulia...

AUNTY POLLY: Nakwepa mitandao ya kijamii kama Ukoma

adminleo