• Nairobi
  • Last Updated March 28th, 2024 11:33 AM
AKILIMALI: Ufugaji kanga unamdumisha kimaisha bila bughudha yoyote

AKILIMALI: Ufugaji kanga unamdumisha kimaisha bila bughudha yoyote

Na CHARLES ONGADI

SIKU njema huonekana asubuhi , ndivyo hali inavyoashiria katika mtaa maarufu wa Makande Railways karibu sana na makazi ya wafanyikazi wa Halmashauri ya Bandari Nchini (KPA) ya Makande, Mombasa.

Hapa tunamkuta Bw Joseph Juma, 51, maarufu kama ‘Jeyjey’ akiwa katika pilkapilka za kila siku za ufugaji wa ndege aina ya kanga.

Bw Juma ambaye ni afisa mshirikishi wa mipango katika shirika la kutetea haki za kibinadamu la Christian Human Rights na pia mshauri wa kisheria katika shirika la Wasioona la Vision of the Blind, ni mfugaji maarufu wa kanga Pwani.

Bw Joseph Juma akiwa na kanga anaofuga katika eneo lake la makazi katika mtaa wa Makande Railways, Mombasa. Picha/ Charles Ongadi

Kanga ni ndege wa jamii ya kuku ambaye mara nyingi huishi porini, mwenye rangi ya kijivu iliyokoza madoadoa meupe.

Bw Juma hata hivyo amevunja mwiko kwani anafuga aina tatu ya kanga, weupe pepepe wenye rangi ya kijivu iliyokoza madoadoa meupe na weusi tititi.

“Ninapenda kufuga aina tofauti ya kanga nikilenga wateja wa aina zote,” asema Bw Juma alipotembelewa na Akilimali hivi majuzi.

Huchukua kipindi cha kati ya miezi minne hadi mitano kwa kanga kukua na kukomaa kabla ya kuanza kutaga mayai akiwa na miezi sita.

Kulingana na Bw Juma, tofauti na kuku, kanga ana uwezo wa kutaga mayai 40 na kuyaangua yote baada ya mwezi mmoja bila hata moja kuharibika.

Bw Juma anasema mara baada kanga kuangua mayai na kupata vifaranga humpa muda wa mwezi mmoja u nusu kisha anawatenganisha na vifaranga hao ili aanze kutaga tena.

Bw Juma anafichua kwamba mbinu hii umhakikishia mfugaji kupata idadi kubwa ya kanga kwa kipindi kifupi.

Mbinu nyingine ya kupata idadi kubwa ya kanga ni kutomwacha kanga kulalia mayai yake pindi muda wa kulalia mayai unapofika.

“Wakati mwingine siachi kanga kulalia mayai yake na badala yake nawapa kuku wa kienyeji kulalia mayai hayo na kanga anapokosa kuona mayai yake anaendelea kutaga mayai zaidi na hata kufikisha 60,” afichua Bw Juma.

Anaongeza kwamba katika kipindi hicho anahakikisha kila kuku wa kienyeji analalia mayai 15 ya kanga hadi pale atakapoyaangua.

Kulingana na Bw Juma, hii inaleta uhusiano thabiti kati ya kanga na kuku ambapo utapata kuku akilea vifaranga vya kanga pasi na bughudha kati yao.

Hupata chakula cha kanga kutoka katika soko kuu la Kongowea ambayo mara nyingi huwa ni nyanya, mboga na wishwa au kununua katika maduka ya vyakula vya mifugo yaliyoidhinishwa.

Aidha, Bw Juma anaiambia AkiliMali kwamba wateja wake wengi ambao huwa ni wenye hoteli kubwa za kitalii mwambao wa Pwani hupenda kununua kanga weupe kuliko wale wa kawaida na weusi.

“Wanavutia na tena nyama yao ni nyororo na tamu kupindukia,” asema Bw Juma.

Anauza kanga mweupe aliyekomaa kwa Sh6,000 wakati kanga mwenye rangi ya kawaida na mwenye rangi nyeusi akichukuliwa kwa Sh3,000.

Wakati biashara inaponoga, ana uwezo wa kuuza kati ya kanga 10 hadi 15 kwa siku.

Hata hivyo, anakiri kwamba amekuwa akikabiliwa na changamoto ya ukosefu wa nafasi ya kutosha ya kuendesha ufugaji wake barabara.

“Niko katikati ya makazi na mara nyingi huwa ni rahisi sana kanga hawa kuibwa pasipokuwa na ungalizi wa kutosha,” asema.

Mkurupuko wa magonjwa mara nyingi humsababishia hasara hasa hatua ya haraka inapokosa kuchukuliwa kuokoa hali.

Anampongeza Gavana wa Mombasa Ali Hassan Joho kwa kumpa sapoti katika ufugaji wake ila anaomba kutengwa kwa eneo wazi kwa ufugaji huu ambao ni nadra kupatikana eneo la Pwani.

Anashauri wafugaji hasa wa ndege mkoani pwani kukumbatia ufugaji wa kanga akisema unalipa vyema huku akishauri vyuo na shule kumtembelea kupata mbinu bora ya ufugaji wa kanga.

You can share this post!

AFYA: Jinsi unavyoweza kukabiliana na mafua

AKILIMALI: Anaona akifika mbali kwenye ukuzaji karakara

adminleo