• Nairobi
  • Last Updated April 23rd, 2024 9:40 PM
Wakenya wengi hawaweki akiba, hukopa marafiki – Ripoti

Wakenya wengi hawaweki akiba, hukopa marafiki – Ripoti

EDWIN OKOTH Na BENSON MATHEKA

WAKENYA wengi wanakabiliwa na hali ngumu ya kiuchumi mwaka huu licha ya serikali kusema hali ya uchumi iko imara.

Kwenye hotuba yake kwa bunge kuhusu hali ya nchi Rais Uhuru Kenyatta alisema uchumi wa Kenya umeimarika kwa asilimia 6.1

Hata hivyo, utafiti wa hivi punde uliofanywa na Benki Kuu ya Kenya na Shirika la FSD Kenya, umeonyesha kuwa hali ngumu ya maisha inawasukuma Wakenya wengi kuomba na kukopa majirani, marafiki na watu wa familia.

Utafiti unasema hali ambayo inalemea watu walioajiriwa ambao wako na umri wa kati ya miaka 27 na 34.

Kulingana na utafiti huo watu wengi wanashindwa kuweka hazina na kukosa kujiandaa kukabiliana na jambo la dharura litatokea.

Utafiti huo ulionyesha kuwa, zaidi ya nusu ya Wakenya wanalalamika hali ya maisha iliwaharibikia 2019, ikilinganishwa na 2018. Wakazi wa maeneo ya mashambani ndio waliathirika zaidi.

“Asilimia 51 ya watu kitaifa waliripoti kuwa hali yao ya kifedha iliharibika 2019, ikilinganishwa na asilimia 23.8 ya watu ambao waliripoti kuwa hali yao iliimarika. Hali ilikuwa mbaya zaidi kwa wakazi wa mashambani, ambapo asilimia 53.3 walisema hali yao iliharibika,” utafiti huo unasema.

Idadi ya watu ambao wamekuwa wakikopa katika maduka ilipanda kutoka asilimia 9.9 mwaka wa 2018 hadi asilimia 29.7 mwaka 2019, huku asilimia 45.4 wakishindwa kulipa na kuathiri wafanyabiashara wadogo.

Kitaifa, watu wanaoorodheshwa kuwa sawa kifedha ni asilimia 21.7 pekee mwaka huu, ikilinganishwa na asilimia 39.4, ilivyokuwa 2016.

Utafiti huo ambao ulihusisha maboma 11,000 katika maeneo ya mijini na mashambani aidha ulibaini kuwa asilimia 62.1 ya Wakenya hawawezi kukimu matumizi yao ya kila siku, ikilinganishwa na mapato yao.

Wanapoishiwa na pesa, watu hao hutafuta marafiki, watu wa familia ama waajiri wao kutafuta msaada kwa sababu hawaweki akiba. Asilimia 24.7 ya wanaowatafuta marafiki huenda kuomba na asilimia 6.5 kukopa.

Asilimia 10.9 huamua kukaa ngumu na kutofanya chochote, japo mtu wa familia aliye na uwezo anaweza kuingilia kati na kuwasaidia.

“Marafiki na familia ndio suluhu kubwa ya kifedha ambayo Wakenya wengi wanatumia wanapoishiwa na pesa kukidhi mahitaji ya kila siku,” utafiti huo unasema.

Utafiti huo ulibaini kuwa, matajiri huwa wanaathirika kifedha wakati mtu wa familia anapofariki, ikilinganishwa na masikini.

Kukosa mikopo na kushindwa kuweka akiba kulitambuliwa kama kunakoharibu hali na kurejesha Kenya nyuma kimaendeleo.

Hali hii inakinzana na ripoti kuwa uchumi wa Kenya umekua kwa asilimia 6.1 katika kipindi cha miezi tisa 2018.

“Wakenya wamekuwa na uwezo wa kupata mapato kwa miaka mingi lakini hawawezi kuweka akiba kwa sababu huwa hawana uhakika wa watapopata pesa. Utafiti unaonyesha kuwa, asilimia 59 ya Wakenya wanalenga kutumia elimu kutimiza ndoto zao kimaisha,” utafiti huo ukasema.

Kwa Wakenya wasio na elimu na wakazi wa mashambani, kutafuta chakula ndilo lengo kuu maishani na kwa wakazi wa mijini afya ndilo lengo kuu.

You can share this post!

Yafichuka magavana hukodisha ofisi na kufanyia kazi Nairobi

Maduka 86 ya dawa yafungwa, dawa za serikali zatwaliwa

adminleo