• Nairobi
  • Last Updated March 29th, 2024 6:25 PM
Ochieng’ hapitiki katika safu ya ulinzi, Mkenya asifiwa Uswidi

Ochieng’ hapitiki katika safu ya ulinzi, Mkenya asifiwa Uswidi

Na GEOFFREY ANENE

WAKENYA David ‘Cheche’ Ochieng’ na Eric Johana Omondi walichezea klabu ya Brommapojkarna na kuisaidia kubwaga Dalkurd 2-0 kwenye mashindano ya Svenska Cupen nchini Uswidi mnamo Februari 25, 2018.

Ochieng’ alicheza dakika zote 90 naye Omondi aliingia kama mchezaji wa akiba mahali pa Marko Nikolic dakika ya 75.

Tovuti ya Brommapojkarna imemsifu Ochieng’. “Pandikizi la mtu Ochieng’ alikuwa hakipitiki katika safu ya ulinzi. Aliwazima wachezaji wa Dalkurd moja baada ya mwingine walipojaribu kumpita wakifanya mashambulizi,” tovuti hiyo imesema.

Wachezaji Marko Nikolic na Martin Rauschenberg walifungia Brommapojkarna mabao ya ushindi dakika za 31 na 51, mtawalia.

Mashabiki 600 walihudhuria mchuano huo katika uwanja wa Grimsta jijini Stockholm. Brommapojkarna, ambayo ilizaba Gefle 2-0 katika raundi ya kwanza, itakutana na miamba Malmo FF katika raundi ijayo mnamo Machi 4, 2018.

Omondi alijiunga na Brommapojkarna kutoka klabu ya Vasalunds IF hapo Januari 1, 2018 kwa kandarasi ya miaka minne.

Naye Ochieng’ alisajiliwa na Brommapojkarna mnamo Januari 12, 2018 kwa kandarasi itakayomweka klabu hiyo hadi Desemba 31, 2020. Alitokea New York Cosmos nchini Marekani alikokuwa amecheza miaka miwili.  Brommapojkarna itashiriki Ligi Kuu mwaka 2018 baada ya kupandishwa daraja. 

You can share this post!

Chepkoech awabwaga wapinzani kwenye IAAF World Indoor Tour

Nakumatt yamumunywa kama pipi na Nkana ya Zambia

adminleo