• Nairobi
  • Last Updated April 20th, 2024 7:55 AM
Mtoto aliyepotea apatikana amefariki ndani ya gari la askofu

Mtoto aliyepotea apatikana amefariki ndani ya gari la askofu

NA MOHAMED AHMED

POLISI jijini Mombasa wanachunguza kifo cha mtoto wa shule ya chekechea aliyepatikana amefariki ndani ya gari la askofu wa kanisa la Ushindi Baptist eneo la Likoni, Mombasa.

Mwili wa Emmanuel Wasike mwenye umri wa miaka sita ambaye ni mwanafunzi wa shule ya Amart Academy ulipatikana Jumatatu asubuhi ukiwa katika viti vya nyuma vya gari hilo lilokuwa limeegeshwa katika uwanja wa kanisa.

Gari hilo aina ya Toyota Allion linamilikiwa na askofu wa kanisa hilo, kulingana na polisi.

Dereva wa kanisa ambaye alikuwa ameenda kubadilisha betri ya gari hilo aliupata mwili wa kijana huyo ukiwa ndani ya gari hilo, kulingana na mshiriki wa kanisa hilo.

Mtoto huyo alikuwa ameripotiwa kupotea mnamo Jumapili na mamake. Akizungumza na Taifa Leo, babake kijana huyo Richar Wasike alisema kuwa mtoto wake hakurudi pale walipokuwa baada ya ibada.

“Kawaida huwa kuna makundi ya ibada yakiwemo yale ya watoto na huwa anaenda kuungana na watoto wenzake na baada kuja kutuunga sisi. Lakini siku hiyo baada ya ibada hatukumona,” akasema Bw Wasike.

Alisema kuwa aliweza kuondoka kanisani hapo akijua kuwa Emmanuel alikuwa na wenzake.

 

Kumtafuta

“Mamake alianza kumtafuta kanisani na baadaje kuja nyumbani akijua kuwa nimeenda naye na alipofika nyumbani ndipo alipojua kuwa sikuwa nimetoka na watoto. Tulienda kanisani kumtafuta na baada tukaripoti polisi,” akasema Bw Wasike.

Jumatatu asubuhi wazazi hao walipigiwa simu kutoka kanisani na kujuzwa kuwa kijana wao amepatikana ndani ya gari akiwa amekufa.

Kulingana na polisi gari hilo lilikuwa halijafungwa. Polisi waliokwenda katika eneo alipopatikana mtoto huyo walisema kuwa mtoto huyo anaonekana kufariki baada ya kukosa hewa wakati alipojifungia ndani ya gari hilo.

Afisa mkuu wa upelelezi enoe la Likoni Henry Ndombi alisema kuwa wameanzisha uchunguzi kuhusiana na kifo cha mtoto huyo they have launched investigations into the incident.

Alisema kuwa tayari wameanza kuwahoji washiriki wa kanisa hilo ambao walikuwepo kanisani siku mtoto huyo alipopotea.

“Mtoto huyo hajaonekana na majeraha yoyote mwilini lakini uchunguzi wetu wa kina utatupa taarifa zaidi,” akasema Bw Ndombi.

Alisema mwili huo umepelekwa katika chumba cha kuhifadhia maiti cha hospitali kuu ya mkoa wa Pwani na unasubiri upasuaji.

You can share this post!

Kalameni afukuzwa kanisani kwa kulemewa kutoa sadaka na...

Raia wa Urusi aliyejitapa hatumii pufya afeli vipimo kwenye...

adminleo