• Nairobi
  • Last Updated April 19th, 2024 8:55 PM
Ashangaza kushangilia kukamatwa kwa mumewe

Ashangaza kushangilia kukamatwa kwa mumewe

Na DENNIS SINYO 

KIMAMA, MLIMA ELGON

WAKAZI wa sehemu hii walishangaa kumuona mama mmoja akishangilia baada ya kupata habari kwamba mumewe alikuwa amekamatwa na polisi wa utawala.

Mama huyo aliabiri pikipiki hadi kituo cha polisi kudhibitisha kwamba mumewe alikuwa amewekwa kwenye seli kwa kupatikana na kwa mama-pima akinywa pombe haramu.

Wengi walitarajia kwamba mama huyo alitaka mumewe kuachiliwa huru lakini wakashtuka kusikia akisema maafisa walikuwa wamefanya jambo zuri sana.

“Huyu mtu alikuwa amenishinda nyumbani na kama mko naye hapa, najua leo nitalala kwa amani bila kusumbuliwa. Najua atabadilisha tabia zake mbaya,” mama huyo alisema.

Yasemekana mumewe alikuwa akipata hela nyingi kazini lakini alikuwa akizitumia vibaya kwa ulevi na anasa jambo ambalo hakufurahia. Licha ya kumsihi kuacha pombe, jamaa alijifanya kiziwi.

Visa vya jamaa kupoteza pesa na wakati mwingine kuibiwa na wenzake kwa mama pima vilimkera mama huyo na akafurahi alipotiwa mbaroni.

Alidai hiyo ilikuwa nafasi bora ya jamaa kupata funzo ili abadilike. “Mama huyo alidai mumewe alikuwa amemea pembe na kuwadharau watu wote waliojaribu kumshawishi kuacha ulevi,” alisema mdokezi.

Aliwataka polisi kumwadhibu abadilike kabla ya kumwachilia.

Kulingana na mdokezi, mama alirejea nyumbani na kumuacha mumewe kwenye seli akisema hiyo ilikuwa nafasi ya pekee ya jamaa kuacha starehe na ulevi.

Wanakijiji waliokuwa hapo walibaki vinywa wazi wakishangaa mama alipowataka polisi kumnyorosha sawasawa badala ya kuwaomba wamuachilie mumewe.

Baadhi walidai akili ya mama haikuwa sawa kwa kuchochea polisi waendelee kumzuilia baba ya watoto wake na kurudi nyumbani.

 

You can share this post!

Uhuru ategwa na wanyakuzi wa ardhi

Mswada wa Waziri Mkuu mwenye mamlaka kuliko Rais...

adminleo