• Nairobi
  • Last Updated April 18th, 2024 2:37 PM
Wakenya kuhesabiwa idadi Agosti 2019

Wakenya kuhesabiwa idadi Agosti 2019

Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Kitaifa la Takwimu (KNBS) Bw Zachary Mwangi. Picha/ Maktaba

Na LUCY KILALO

SHIRIKA la Kitaifa la Takwimu (KNBS) linapanga kuendesha shughuli ya kitaifa ya kuhesabu watu Agosti mwaka 2019.

Mkurugenzi Mkuu wa KNBS, Bw Zachary Mwangi alisema shughuli hiyo itagharimu Sh18.5 bilioni, ambapo itahusisha wafanyakazi 170,000.

Bw Mwangi aliiambia kamati ya Bunge la Kitaifa ya Kufuatilia Utekelezaji wa Masuala ya Kikatiba, kwamba shughuli yenyewe itafanywa Agosti 24 na 25 mwaka ujao, ingawaje mwigo wake utafanywa tarehe hizo mwaka huu.

Japo watu watahesabiwa 2019, Wakenya watasuburi kwa karibu mwaka moja kupata matokeo kamili.

“Matokeo ya mapema yatatolewa katika muda wa mwezi moja, ripoti ya kimsingi baada ya miezi mitatu, na ripoti yenye taarifa kamili na tathmini kutolewa baada ya miezi 12,” alieleza Bw Mwangi.

Maswali kadha yaliibuka katika kikao cha jana, ambapo mbunge wa Kajiado Mashariki, Bi Peris Tobiko alitaka kujua ikiwa utaratibu huo utawajumuisha waliozaliwa na jinsia zote mbili, kuwa na maelezo ya kuaminika hasa baada ya utata ulioibuka kuhusiana na matokeo ya hesabu ya watu ya 2009 na iwapo teknolojia wanayonuia kutumia itakuwa ya kutegemewa.

Matokeo ya hesabu ya watu ya 2009 yalionyesha kulikuwa na takriban watu 38.6 milioni nchini.
Hesabu ya mwaka ujao itatumiwa katika ugawaji wa raslimali.

 

You can share this post!

Uchomaji makaa wapigwa marufuku Narok

Miili ya maafisa wawili kutoka Bomet yapatikana Homa Bay

adminleo