• Nairobi
  • Last Updated March 29th, 2024 6:25 PM
TAHARIRI: Heko Spika Muturi kukataa ombi tata

TAHARIRI: Heko Spika Muturi kukataa ombi tata

Spika wa Bunge la Kitaifa Justin Muturi. Picha/ Maktaba

NA MHARIRI

SPIKA wa Bunge la Taifa, Bw Justin Muturi, Jumanne alitumia busara kwa kukataa ombi la wakili Adrian Kamotho Njenga la kutaka wabunge wamuondoe Jaji Mkuu David Maraga na makamishna wengine sita wa Tume ya Huduma ya Mahakama (JSC).

Bw Muturi alisema Bw Njenga angewasilisha ombi lake mbele ya JSC ambayo ni tume ya kikatiba iliyotwikwa jukumu la kupokea malalamishi yote kuhusu maafisa wa Mahakama akiwemo Jaji Mkuu David Maraga na kuchukua hatua kwa mujibu wa sheria zilizopo.

Ulikuwa uamuzi wa busara na wa hekima ambao ulizima tetesi kwamba hatua ya Bw Njenga ilikuwa njama ya Jubilee ya kuadhibu Mahakama kwa kutotoa maamuzi yanayopendelea serikali.

Uamuzi wa Bw Muturi umezuia bunge kutumiwa vibaya na watu wanaotaka kugonganisha mihimili mitatu ya serikali; Bunge, Mahakama na Serikali Kuu.

Tunasema hivyo kwa sababu akiwa wakili, Bw Njenga anaelewa jukumu la JSC na japo alilenga makamishna wa tume hiyo, kuna utaratibu aliopuuza makusudi kwa msukumo wa kujitanua kwamba aliangusha majaji iwapo ombi lake lingekubaliwa na kufaulu.

Kumekuwa na tabia ya watu kadhaa ya kutaka kutumia asasi za serikali kulipiza kisasi dhidi ya wanaohisi kuwa wapinzani au kikwazo kwao.

Hii ni tabia inayopaswa kukomeshwa kwa kila hali na Bw Muturi alifaulu kwa hilo alipozima ombi la Bw Njenga.

Kuna haja ya kila asasi ya serikali kuwa makini katika kila hatua inayochukua na kufahamu kwamba inaweza kufanya makosa yanayoweza kuathiri nchi kwa miaka mingi.

Kwa kutowasilisha ombi hilo kwa kamati husika ya bunge, Bw Muturi alionyesha kwamba anaweza kulinda uhuru wa bunge kwa kutoruhusu miswada na mijadala inayoenda kinyume na katiba.

Aidha, alionyesha kwamba japo wabunge wengi ni wa Jubilee, bunge linaweza kukataa kutumiwa kutia muhuri maazimio ya serikali kwa kupitisha miswada inayoenda kinyume cha katiba.

Bw Muturi alisaidia kuiondolea serikali tuhuma ambazo baadhi ya wananchi walikuwa wameanza kuzitoa, kwamba hatua hiyo ni ile ahadi ya kuifunza adabu idara ya Mahakama.

Huu ndio mwelekeo ambao tunatarajia kutoka kwa viongozi na maafisa wa serikali ambao waliapa kulinda, kutetea na kuheshimu katiba yetu.

 

 

You can share this post!

Miili ya maafisa wawili kutoka Bomet yapatikana Homa Bay

FATAKI: Ukiachwa kubali yaishe, hii tabia ya kitoto ya...

adminleo