• Nairobi
  • Last Updated April 23rd, 2024 11:14 AM
‘Team Komboa Kenya’ yajitokeza kukabili ‘Tangatanga’ na ‘Kieleweke’

‘Team Komboa Kenya’ yajitokeza kukabili ‘Tangatanga’ na ‘Kieleweke’

Na DERICK LUVEGA

SIKU moja baada ya mkutano wa kundi la ‘Kieleweke’kutibuka mjini Kakamega, vuguvugu jingine la kisiasa limejitokeza ili kuyakabili makundi ya ‘Kieleweke’ na ‘Tanga Tanga.’

Kundi hilo, linalojiita ‘Team Komboa Kenya’ linahusishwa na kiongozi wa Chama cha Amani (ANC) Musalia Mudavadi.

Duru zilisema kundi hilo lilibuniwa na washirika wa karibu wa Bw Mudavadi, baada ya mikutano kadhaa ya faragha.

Mbunge wa Sabatia, Alfred Agoi, ambaye ni mshirika wa karibu wa Bw Mudavadi, alithibitisha kubuniwa kwa kundi hilo.

Kwenye mahojiano na ‘Taifa Jumapili’, Bw Agoi alisema kiongozi huyo anafanya mikutano kadhaa jijini Nairobi, ili kuweka mikakati ya uzinduzi wa kundi hilo jijini Kakamega “hivi karibuni.”

Bw Agoi alisema makundi hayo mawili yalibuniwa kumuunga mkono au kumpinga Naibu Rais William Ruto, lakini kundi la ‘Team Komboa Kenya’ litapigania maslahi ya Wakenya.

Mkutano wa kundi la ‘Kieleweke’ ambalo linampinga Dkt Ruto, ulipangiwa kuandaliwa jana mjini Kakamega.

Chama cha Ford-Kenya tayari kimejitenga kuhusika kwa vyovyote katika maandalizi ya mkutano huo. Ilidaiwa kwamba kiongozi wake, Moses Wetang’ula ni miongoni mwa viongozi ambao wangehudhuria.

Duru zilieleza kuwa Bw Mudavadi alitarajiwa kuwa mwalikwa mkuu katika mkutano huo, ambapo angetoa mwelekeo rasmi wa kisiasa wa ukanda wa Magharibi.

Duru zilieleza kuwa, Bw Mudavadi alifutilia mbali mkutano huo dakika za mwisho mwisho, ili kumruhusu kila mmoja kuhudhuria, kwani wanasiasa wengi waliotarajiwa walikuwa mbali.

Na jana, waandani wa Bw Mudavadi walidai mkutano huo ulipangwa na Seneta Cleophas Malala wa Kakamega na mbunge maalum Godfrey Osotsi, wakilenga kuutumia kutafuta muafaka kati ya Otsosi na Mudavadi.

You can share this post!

Uhuru amkausha Ruto kwenye uteuzi

Jina langu si tiketi ya Ikulu, Ruto aambia wapinzani

adminleo