• Nairobi
  • Last Updated April 25th, 2024 12:26 PM
‘Tangatanga’ na ‘Kieleweke’ wakosa adabu kuraruana kanisani

‘Tangatanga’ na ‘Kieleweke’ wakosa adabu kuraruana kanisani

Na CHARLES WASONGA

MGAWANYIKO ndani ya chama cha Jubilee uliendelea kushuhudiwa Jumapili pale kundi la wabunge wanaegemea mrengo wa Rais Uhuru Kenyatta (Kieleweke) na Naibu wake William Ruto (Tangatanga) walipofarakana katika kanisa moja katika eneobunge la Naivasha.

Hafla ya kutoa shukrani katika Kanisa la AIPCA mjini Naivasha iligeuka kuwa uwanja wa mirengo mahasimu ha  kunyoosheana kidole cha lawama na kurushiana cheche za maneno.

Vurugu zilianza baada ya kundi la ‘Kieleweke’ likiongozwa na Mbunge wa Nyeri Mjini Ngunjiri Wambugu, Joshua Kuttuny (Cherangany) na Gathoni Wa Muchomba (Mbunge Mwakilishi, Kiambu) na wengine walipowasili katika kanisa hilo bila kumfahamisha Mbunge wa eneo hilo Jane Kihara ambaye ni mwandani wa Dkt Ruto.

Isitoshe, wabunge hao walimshambulia Naibu Rais, na wabunge wanaomuunga mkono, hatua iliyomkera Bi Kihara ambaye alikuwepo kanisani humo.

Bw Wambugu ndiye alikuwa wa kwanza kumshutumu Naibu Rais kwa kumhujumu Rais Kenyatta badala ya kufanya kazi walivyowaahidi raia.

Alisema wanachama wa kundi lake wako nyuma ya Rais Kenyatta na kuwa hawatakaa kitako na kutizama huku Dkt Ruto akiendelea kuunga mkono wafisadi.

“Rais alituita sote baada ya uchaguzi na tukakubaliana kulenga maendeleo lakini miezi michache baadaye watu wengine wakaanza kuongea kuhusu uchaguzi wa 2022,” akasema.

Kauli yake iliungwa mkono na Bw Kuttuny aliyesema kuwa chama cha Jubilee kimegawanyika katika mirengo miwili, moja inaunga mkono vita dhidi ya ufisadi na nyingine inaunga mkono Dkt Ruto anayetetea washukiwa wa ufisadi.

Alishangaa ni kwa nini Naibu Rais anakula na kuwatetea magavana wa Samburu na Kiambua ambao wametuhumiwa kwa wizi wa pesa za umma.

“Tangu Rais Kenyatta na kiongozi wa upinzani Raila Odinga waliporidhiana kisiasa taifa hili limekuwa tulivu lakini watu wengine wanaounga mkono ufisadi hawaoni hii,” akasema.

Na Wa Muchomba aliwashambulia wabunge wanaomuunga mkono Ruto alisema haja yao ni kujitajirisha kwa kutumia pesa za umma zilizoibwa.

Alimsuta Ruto kwa kumhujumu Rais akiongeza kuwa wabunge kutoka eneo la Mlima Kenya hawatanyamaza ila watamkemea.

“Kuna Rais mmoja pekee nchini na hakuna aliyeruhusiwa kumdhalilisha kwa njia yoyote,” akasema.

Lakini alipoamka kuongea, Bi Kihara aliyeonekana mwenye hasira aliwasuta wenzake kwa kumkosea heshima Naibu Rais akisema kuwa hawajuti kumuunga mkono Dkt Ruto.

Aliwakashifu wabunge wa eneo la Mlima Kenya akiwataka kukoma kujaribu kugawanya Rift Valley akiongeza kuwa Dkt Ruto hajaanza kampeni kama wanavyodai.

“Wabunge kutoka Kati mwa Kenya wanafaa kusalia maeneo yao na wakome kuelekeza kuhusu yule tunapaswa kuuunga mkono kwani sisi sio washenzi,” Bi Kihara akasema kwa ghadhabu.

You can share this post!

Moi amshangaa Ruto kuanza kampeni za 2022

Ziara ya Raila nyumbani kwa Oparanya yaibua maswali

adminleo