• Nairobi
  • Last Updated April 19th, 2024 8:55 PM
Atoroka baada ya kuua mtu na kunywa damu yake

Atoroka baada ya kuua mtu na kunywa damu yake

Na JADSON GICHANA na PETER MBURU

POLISI katika kaunti ya Kisii wanamsaka mwanamume aliyemuua mwenzake kwa kumfuma mkuki kifuani na kunywa damu yake.

Mkuu wa polisi wa Gucha Kusini, Bw Moses Kanyi alisema mshukiwa aliyetambuliwa kama Kennedy Keraka, 45, alitorokea Trans Mara baada ya kumuua Bw Daniel Obara.

Mke wa marehemu, Bi Risper Kwamboka Obara, alisema mumewe alitoka nyumbani jioni na kumweleza kuwa alikuwa akienda kudai pesa zake.

“Mume wangu aliniaga kuwa alikuwa akienda kudai pesa kutoka kwa mtu aliyemuuzia kikapu cha kuchunia majani chai. Baada ya masaa mawili, nikasikia kelele kwa majirani kuwa mume wangu amekufa,” akasema.

Bw Kanyi alisema wananchi waliojawa na hasira baada ya tukio hilo, walizichoma nyumba mbili za mshukiwa na kuharibu mimea iliyokuwa shambani mwake.

Kwingineko mjini Nakuru, mwanamume anayetuhumiwa kumuua shemeji yake wakipigania shati, jJumanne alijitetea kuwa marehemu alikuwa rafikiye mkubwa na kwamba alikufa kwa bahati mbaya.

Joel Mesheti Esho, 31, anatuhumiwa kumuua Bw Joel Mpapa Murumbi ambaye alikuwa mume wa dadake mnamo Mei 15, 2013, ikidaiwa walikuwa wakizozania shati.

Mashahidi awali walikuwa wamemweleza Jaji Maureen Odero kuwa mshtakiwa alimvamia marehemu kwa gongo walipokuwa wakipigana, mshukiwa akitaka kutwaa shati alilokuwa amevalia marehemu. Ndipo mshtakiwa alipompiga kwa gongo hilo kichwani.

Daktari aliyemfanyia marehemu upasuaji alisema kifo cha Mpapa kilitokana na majeraha kisogoni kwa sababu ya kupigwa na kifaa butu, wala si kuangukia jiwe kama alivyojitetea mshukiwa.

Kesi hiyo itaamuliwa Mei 4, mwaka huu.

You can share this post!

Wazazi: Vitabu hivi vinawapotosha wanafunzi, viondolewe

‘Marehemu alifichua waliomuua kabla ya kufa’

adminleo