• Nairobi
  • Last Updated March 29th, 2024 7:50 AM
Polo aachilia mkojo ndani ya basi safarini

Polo aachilia mkojo ndani ya basi safarini

Na TOBBIE WEKESA

TULIENGE, BUNGOMA

ABIRIA waliokuwa wakisafiria basi moja walipigwa na mshangao baada ya polo kuachilia mkojo ndani ya gari dereva alipokataa kusimamisha gari ili ajisaidie.

Duru zinasema polo alikuwa amelalamika kubanwa na mkojo kwa muda mrefu. Alimuomba utingo amueleze dereva asimamishe gari ili atulize hali. Inadaiwa baada ya kuelezwa na utingo kuhusu ombi la abiria, dereva aliongeza kasi ya gari akimtaka jamaa avumilie hadi mwisho wa safari.

Polo aliamua kumsongea dereva na kumueleza mwenyewe. “Dereva tafadhali simamisha gari kidogo. Nimebanwa sana,” polo alimueleza dereva.

Duru zinasema dereva alimuangalia polo na kuongeza mwendo wa gari. “Ukipanda gari hukujua haina choo. Mimi sisimamishi gari. Jisoti,” dereva alimueleza polo.

Kulingana na mdokezi, polo alirudi kwenye kiti chake na kuachilia mkojo bila wasiwasi wowote ukatapakaa garini.

“Dereva ameniambia yeye hatasimamisha gari kwa hivyo nijisoti,” polo alisema huku mkojo ukiendelea kumtoka.

Utingo alimuamrisha dereva kulisimamisha gari mara moja. Gari lilisimamishwa na polo akaamrishwa atoke nje. “Mbona unasimamisha gari? Shida iko wapi? Mimi nimejisoti ulivyonieleza,” polo alimuambia dereva huku abiria wakiangua vicheko.

Utingo alianza kumzomea polo. “Wewe ni mtu wa aina gani? Huna aibu hata kidogo kutoa kifaa chako na kukojoa hadharani mbele ya umma,” utingo alimzomea polo.

Dereva naye alimuamrisha polo aoshe mkojo garini mara moja. “Sitaki ujinga wenu. Mimi si rika lenu. Nilipowaomba msimamishe gari si mlikataa. Makosa si yangu,” polo naye aliwakemea dereva na utingo na kuungwa mkono na baadhi ya abiria.

 

You can share this post!

WANDERI: Falsafa ya Mbaya Wetu inaliponza taifa hili letu

NYOTA YAKO: MACHI 07, 2018

adminleo