• Nairobi
  • Last Updated March 28th, 2024 1:29 PM
KIFO CHA NASA: Dalili zote za muungano kusambaratika

KIFO CHA NASA: Dalili zote za muungano kusambaratika

Na CHARLES WASONGA

MKUTANO kati ya Rais Uhuru Kenyatta na kiongozi wa NASA Raila Odinga sasa unaonekana kupanua ufa katika muungano wa NASA baada ya vinara wenzake kulalamikia kutohusishwa.

Jumamosi, Mbw Kalonzo Musyoka, Musalia Mudavadi na Moses Wetang’ula walitumia maneno makali na mazito kuelezea ghadhabu zao.

Walisema hawakuwa na habari kuhusu mazungumzo hayo waliyotaja kama ya “watu wawili na NASA haikuwakilishwa kwa njia yoyote ile”.

“Masuala ambayo NASA imekuwa ikipigania kama vile haki katika uchaguzi na utawala bora hayakuangaziwa katika mazunguzo hayo.

NASA imekuwa ikiitisha mazungumzo ya kitaifa yanayowajumuisha wadau wote kwa maslahi ya Wakenya; sio maafikiano kati ya watu wawili,” Bw Mudavadi akasema kwenye kikao na wanahabari mjini Mombasa Jumamosi.

Naye Bw Musyoka alisema katika mkutano wao kesho, watataka maelezo zaidi kutoka kwa Bw Odinga kuhusu mkutano wake na Rais Kenyatta.

“Mkutano wetu wa Jumatatu unatupa nafasi nzuri ya kujadili masuala haya yote katika muktadha mwafaka.

Wale wenye macho wanaweza kuona na wale wenye masikio wanaweza kusikia. Naacha suala hilo hapo huku nikisubiri mkutano wa Jumatatu,” akasema.

Hata hivyo, wabunge na viongozi wengine wa Wiper walimshutumu Bw Odinga wakisema aliwasaliti vinara wenzake kwa kukutana na Rais Kenyatta bila kuwahusisha.

Bw Wetangula alimtaka kinara huyo wa ODM kujitayarisha kwa maelezo ya kina wakati wa mkutano wao wa kesho.

“Raila atatueleza kwa nini hatukuhusisha na nini walichokizungumza na Uhuru,”alisema Bw Wetangula.

 

Wakome kuteta

Hata hivyo, Naibu Rais William Ruto aliwataka vinara hao wakome kuteta na badala yake wajiunge na Bw Odinga kuunga serikali. “Mkutano wa Raila na rais uliashiria kikomo cha msimu wa siasa.

Naomba wenzangu katika upinzani wakome kuteta kuwa hawakuhusishwa na badala yake waje tujenge Kenya pamoja,”alisema Bw Ruto.

Duru ziliambia Taifa Jumapili kwamba mikakati kuhusu mkutano huo, uliowashangaza wengi, ilianza kuandaliwa wiki kadhaa zilizopita. Lakini mipango hiyo ilishika kasi Alhamisi wiki iliyopita ilipobainika kuwa Waziri wa Mashauri ya Kigeni wa Amerika Rex Tillerson angefika nchini kwa ziara ya siku tatu.

“Usiri mkubwa uligubika maandalizi ya mkutano huo. Ni msaidizi wa Rais Jomo Gecaga na bintiye Raila Winnie Odinga pekee ambao walikuwa katika mstari wa mbele katika maandalizi hayo,” mshirika mmoja wa Odinga alisema.

Hata hivyo, mnamo Alhamisi wiki jana Rais Kenyatta na Naibu wake William Ruto walijadiliana kuhusu mkutano huo, kabla ya Rais mwenyewe kumfikia Bw Odinga kwa simu na wakapanga kukutana Ijumaa asubuhi.

 

You can share this post!

Kioja mwizi wa pikipiki kuirejesha huku akilia

Wagonjwa KNH kuanza kuwekewa vibandiko

adminleo