• Nairobi
  • Last Updated April 25th, 2024 5:29 PM
Wavuvi wa Kenya wavamiwa tena na polisi wa Uganda

Wavuvi wa Kenya wavamiwa tena na polisi wa Uganda

Na KNA

WAVUVI 20 wa Kenya walivamiwa Alhamisi usiku na kunyang’anywa taa zao zinazokadiriwa kuwa za thamani ya Sh70,000 na maafisa wa usalama wa Uganda katika Ziwa Victoria.

Wavuvi hao kutoka ufuo wa Kinda, kaunti ndogo ya Suba Kusini walishikwa walipoenda kuvua Omena.

Mwanachama wa kamati simamizi ya ufuo huo wa Kinda, Bw Boni Sidika alisema tukio hilo lilifanyika wakati maafisa watatu wa usalama ambao walikuwa na bunduki walivamia boti tano zilizokuwa zimebeba wavuvi wanne kila moja.

Alisema wavuvi hao waliumizwa walipojaribu kujitetea kwa kueleza kuwa walikuwa wakivua katika maji ya Kenya.

Bw Wycliffe Aila, mmoja wa wamiliki wa boti hizo na taa, alisema maafisa hao walijaribu kwanza kuchukua taa za kuvua lakini wavuvi walipokataa waliwapiga.

“Waliwaumiza wavuvi kwa kutumia mbao baada ya wavuvi hao kukataa kuhangaishwa. Wavuvi hao walijeruhiwa sehemu kadha mwilini,” Bw Aila alieleza.

Alisema wavuvi hao pia walilazimishwa kutupa majini samaki waliokuwa wamevua. Wavuvi hao sasa wanataka serikali itatue mzozo wa mipaka ya ziwa hilo kati ya Kenya na Uganda.

“Tunasihi serikali itafute suluhisho la kudumu kwa mizozo inayohusu mpaka kati ya Kenya na Uganda,” Bw Sidika alisema.

OCPD wa Suba Kusini, Bw Paul Kipkorir alisema wavuvi hao hawajaandikisha taarifa kwa polisi.

“Hakuna mvuvoi ameandikisha taarifa lakini tunaulizia ili tuweze kufanya uchunguzi kuhusu tukio hilo,” alisema Bw Kipkorir.

 

 

You can share this post!

Ziara ya Rais Uhuru na Raila mjini Kisumu yaahirishwa

Msituhusishe kwa mzozo wenu, Mutula awaambia vinara wa NASA

adminleo