• Nairobi
  • Last Updated April 19th, 2024 8:55 PM
27 wakamatwa kufuatia ghasia Kakamega

27 wakamatwa kufuatia ghasia Kakamega

Na SHARON OKOLLA

Watu 27 walikamatwa mjini Kakamega kwa kuhusika katika rabsha baada ya waombolezaji kukabiliana na polisi wa kupambana na fujo.

Machafuko yaliibuka mjini wakati mwili wa Sharlyne Mwanzia ulipokuwa ukitolewa chumba cha kuhifadhia maiti kupelekwa nyumbani kwao, mtaa wa Scheme mjini humo.

Vitoa machozi vilirushwa na milio ya risasi ilisikika wakati vijana walikuwa wakiandamana kuwataka maafisa wa polisi kumkamata mshukiwa wa mauaji hayo.

Msimamizi wa polisi eneo la Kakamega Joseph Chebii Jumamosi alithibitisha kukamatwa kwa washukiwa hao 27. Alisema watafikishwa mahakamani Jumatatu.

Hata hivyo, alikana madai kwamba baadhi ya vijana walifyatuliwa risasi na maafisa wa polisi Ijumaa.

“Hakuna ripoti iliyowasilishwa kwetu kuhusiana na suala hilo kufikia sasa, kwamba kuna mtu aliyejeruhiwa wakati wa vurugu iliyoshuhudiwa Ijumaa,” alisema.

“Hata hivyo, maafisa wawili wa polisi walijeruhiwa kidogo walipopigwa kwa mawe na vijana waliokuwa na ghadhabu,” aliongeza.

Aliwashauri wakazi wa eneo hilo kuepuka kukabiliana na maafisa wa polisi. Bw Chebii alisema wanawataka washukiwa kuwapa habari zaidi ambayo inaweza kupelekea kukamatwa kwa washukiwa zaidi.

Alishutumu mashambulizi dhidi ya maafisa wa polisi. Waombolezaji walionekana kulemewa na hisia kwani walilia kwa uchungu mwingi na kushutumu mauaji hayo ya mtoto huyo wa miaka tisa.

Mtoto huyo aliuawa na mwili wake kutupwa ndani ya tanki la maji, nyumbani kwao. Sharlyne aliyekuwa mwanafunzi wa darasa la tatu katika Shule ya Msingi ya St Joseph’s Academy, alipotea nyumbani kwao Machi 11, 2018 alipokuwa akicheza na ndugu zake. Mwili wake ulipatikana Machi 16.

Waombolezaji hao waliwashtumu polisi kwa kushindwa kukabiliana na ongezeko la ukosefu wa usalama .

Msichana huyo wa darasa la tatu katika shule ya St Joseph’s Academy, Kaunti ya Kakamega, alitoweka nyumbani kwa wazazi wake siku 13 zilizopita na anashukiwa kuhadaiwa na mtu asiyejulikana.

Ijumaa, vurumai zilizuka baada ya kundi la vijana kuanza kuharibu nyumba ambapo mwili wa mtoto huyo uligunduliwa, waombolezaji walipokuwa wakikaribia mtaa huo.

Mtu mmoja alijeruhiwa mikono alipojaribu kuchukua mkebe wa gesi hiyo ya kutoza machozi walipokuwa wakikabiliana na polisi.

Mkuu wa Polisi Kaunti, Bw Johanah Tonui hata hivyo alipuuzilia mbali mdai hayo akisema kuwa polisi walitumwa kuwatawanya vijana ambao walikuwa wakipora kutoka kwa duka kuu.

“Kile tulichofanya ni kuwatawanya vijana waliokuwa wamezuia barabara na kuwapiga mawe maafisa ili kuwachanganya akili na kisha kupora,” alitetea afisa.

You can share this post!

Atakayefichua mwanamume anayewatapeli wabunge kutuzwa...

Uchunguzi waanika uozo unaokumba shule za umma

adminleo