• Nairobi
  • Last Updated March 28th, 2024 11:33 AM
Starlets waumiza She-polopolo 3-0 kwao nyumbani

Starlets waumiza She-polopolo 3-0 kwao nyumbani

Na GEOFFREY ANENE

HARAMBEE Starlets ya Kenya imetuma onyo la mapema kwa wapinzani wake wa raundi ya kwanza ya mechi za kufuzu kushiriki Kombe la Afrika mwaka 2018 kwa kupepeta wenyeji Zambia 3-0 katika mechi ya kirafiki uwanjani Arthur Davies mjini Kitwe, Jumapili.

Kenya, ambayo itaalika Uganda mjini Machakos mnamo Aprili 4 na kupiga mechi ya marudiano Aprili 8 ugenini, imezima She-polopolo kupitia mabao ya Mwanahalima ‘Dogo’ Adam na Corazone Aquino.

Mvamizi hodari Adam aliipa Starlets uongozi dakika ya 18 kabla ya kiungo Aquino kuzamisha chombo cha Zambia kabisa na mabao mawili dakika 10 za mwisho.

Ni kisasi kitamu dhidi ya Zambia kwa sababu warembo wa kocha David Ouma walilazwa 4-2 kwa njia ya penalti katika mechi ya kutafuta mshindi wa medali ya shaba kwenye mashindano ya Cosafa mwaka 2017.

Starlets ilitumia mchuano huu kujipiga msasa kabla ya kulimana na Uganda.

Ikibandua Uganda nje, Kenya itamenyana na mabingwa wa Afrika mwaka 2008 na 2012 Equatorial Guinea katika raundi ya pili Juni 4 na Juni 9. Mshindi wa raundi ya pili atajikatia tiketi ya kushiriki Kombe la Afrika litakalofanyika Novemba 17 hadi Desemba 1 katika miji ya Accra na Cape Coast.

Starlets ilipepeta Uganda 4-0 mjini Jinja zilipokutana katika mechi ya makundi ya mashindano ya Afrika Mashariki na Kati (Cecafa) Septemba mwaka 2016.

Esse Akida, ambaye alifunga mabao mawili katika mechi hiyo, alikosa ziara ya Zambia kwa sababu ya jeraha, lakini Ouma ni mwingi wa matumaini kwamba mshambuliaji huyu atapata afueni kabla ya kukutana na Uganda.

Kenya ilishiriki Kombe la Afrika kwa mara yake ya kwanza kabisa mwaka 2016 nchini Cameroon.

Ilijikatia tiketi ya kuelekea Cameroon baada ya mpinzani wake wa raundi ya kwanza Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo kujiondoa. Ililemea Algeria katika raundi ya pili kupitia mabao ya ugenini baada ya kutoka 2-2 nchini Algeria na 1-1 jijini Nairobi.

Ikiwa itapiga Uganda katika raundi ya kwanza, Starlets itavaana na mabingwa wa zamani wa Afrika Equatorial Guinea katika raundi ya pili Juni. Mshindi wa raundi ya pili ataingia Kombe la Afrika litakalofanyika Novemba 17 hadi Desemba 1 katika miji ya Accra na Cape Coast.

Vikosi: 

Kenya – Wachezaji 11 wa kwanza – Pauline Atieno, Pauline Musungu, Wincate Kaari, Lilian Adera, Dorcas Shikobe, Caroline Omondi, Cheris Avilia, Cynthia Shilwatso, Neddy Atieno, Wendy Ann Achieng na Mwanahalima Adam; Wachezaji wa akiba – Maureen Shimuli, Vivian Nasaka, Caroline Kiget, Vivian Corazone Aquino, Mercy Achieng, Doris Anyango na Sheryl Angachi.

Zambia – Wachezaji 11 wa kwanza – Catherine Musonda, Mary Mwakapila, Theresa Chewe, Misozi Zulu, Rhoda Chileshe, Hellen Chanda, Margaret Belemu, Lweendo Chisamu, Jacqueline Nkole, Jane Chalwe na Racheal Kundananji

You can share this post!

Pasta aalika mganga atibu wanawe walevi

BI TAIFA MACHI MOSI, 2018

adminleo