• Nairobi
  • Last Updated April 19th, 2024 7:55 AM
Mkali wa kriketi motoni kwa kubadilisha hali ya mpira kwa manufaa yake

Mkali wa kriketi motoni kwa kubadilisha hali ya mpira kwa manufaa yake

Na GEOFFREY ANENE

MCHEZAJI wa kriketi wa Australia, Steve Smith amepigwa marufuku mechi moja na kupoteza Sh1, 435,408 baada ya kupigwa faini ya asilimia 100 kwa sakata ya kubadilisha hali ya mpira ili kujinufaisha Machi 24, 2018.

Cameron Bancroft, ambaye ni mchezaji mwenza, alikwepa marufuku, lakini akapigwa faini ya Sh1, 076,556 (asilimia 75 ya ada yake ya mechi) baada ya kupatikana akidanganya mchezoni kwa kusugua mpira ili kufanya Australia iwe na kazi rahisi kupata pointi dhidi ya wenyeji Afrika Kusini mjini Cape Town.

Bancroft, 25, alinaswa kwenye runinga akiwa na kifaa fulani akisugua mpira kabla ya kukificha katika mfuko wa long’i yake.

Smith, 28, alipokonywa unahodha wa Australia kutokana na kisa hicho. David Warner, 31, pia alijiuzulu majukumu ya naibu ya nahodha. Inaaminika wachezaji hawa viongozi walimsukuma Bancroft kuvunja sheria hiyo.

Akizungumzia hatua ya kuadhibu Smith na Bancroft, Afisa wa marefa kutoka Shirikisho la Kriketi duniani (ICC) Andy Pycroft alisema, “Kubeba kifaa ambacho si cha mchezo wa kriketi uwanjani kwa nia ya kubadilisha hali ya mpira ili kukuwezesha kushinda mpinzani wako ni kinyume na sheria na pia inavunja maadili ya mchezo huu.”

Mwaka 2016, raia wa Afrika Kusini Faf du Plessis alijipata pabaya dhidi ya Australia mjini Hobart akijaribu kubadilisha hali ya mpira kwa kutumia mate akiwa na peremende kinywani. Alipoteza asilimia ya ada ya mechi, ingawa aliepuka marufuku.

You can share this post!

Maumivu ya tumbo hayapo tena, Kipsang’ ashinda...

Ajenti wa M-Pesa kizimbani kuhusu njama ya kumtapeli Sabina...

adminleo