• Nairobi
  • Last Updated April 25th, 2024 7:25 PM
Ajenti wa M-Pesa kizimbani kuhusu njama ya kumtapeli Sabina Chege

Ajenti wa M-Pesa kizimbani kuhusu njama ya kumtapeli Sabina Chege

Na RICHARD MUNGUTI

AJENTI wa Mpesa wa kampuni ya Safaricom Jumatatu alishtakiwa kwa kusajili nambari ya simu ya mbunge mwakilishi wa wanawake kaunti ya Murang’a Bi  Sabina Chege kwa lengo la kumlaghai pesa pamoja na wabunge wengine katika kashfa ya kimitandao.

Catherine Nyaboke Omwene ameshtakiwa siku 12 baada ya wanafunzi wawili wa chuo kikuu kufunguliwa shtaka la kujaribu kupokea Sh100,000 kutoka kwa aliyekuwa Mbunge wa Gem Jakoyo Midiwo.

Bi Omwene alifikishwa mbele ya hakimu mwandamizi katika mahakama ya Milimani Bi Martha Mutuku. Alikabiliwa na mashtaka matano ya ufisadi wa kimitandao na kujaribu kumtapeli Bi Chege.

Kiongozi wa mashtaka Bi Pamela Veda alimweleza hakimu kwamba kabla ya kukamatwa kwa mshtakiwa wabunge walikuwa wamelalamika kwa polisi kwamba nambari zao zinatumikiwa na walaghai kujipatia mamilioni ya pesa kutoka kwa wananchi na wabunge.

“Wabunge walidai wamefujwa mamilioni ya pesa na matapeli,” alisema Bi Veda.

Mshtakiwa ambaye hakuwa na wakili wa kumtetea alidaiwa mnamo Machi 3, 2018 katika duka la kuuza bidhaa za urembo za wanawake lijulikano Update Beauty Shop katika mtaa wa Donholm kaunti ya Nairobi aliandikisha nambari ya simu ya Bi Chege.

Bi Omwene aliandikisha nambari ya mbunge huyo kwa mmoja Bw Waziri Benson Masubo. Shtaka lilisema mshtakiwa alikuwa na lengo la kuwatapeli umma alipoandikisha simu hiyo ya Bi Chege kwa jina la Bw Masubo.

Bw Omwene alikabiliwa na shtaka la kukubali sajili ya Safaricom itumike kwa njia ya uwongo kwa kuandikisha nambari ya Bi Chege kwa jina la Bw Masubo.

Mshtakiwa alikanusha mashtaka yote na kuomba aachiliwe kwa dhamana. Bi Mutuku aliamuru mshtakiwa alipe dhamana ya pesa tasilimu Sh100,000 na kuorodhesha kesi isikizwe Aprili 26, 2018,

Korti iliamuru upande wa mashtaka umkabidhi mshtakiwa nakala za mashahidi aandae utetezi wake.

Wanafunzi wa chuo kikuu cha Multi-Media Mabw Derick Kimutai Ng’etich na Edwin Ndiritu walikana walijaribu kumlaghai Bw Midiwo wakijifanya wametumwa na Bi Chege kupokea Sh100,000.

You can share this post!

Mkali wa kriketi motoni kwa kubadilisha hali ya mpira kwa...

Mamaye Wanyama abwagwa uchaguzini

adminleo