• Nairobi
  • Last Updated March 28th, 2024 5:22 PM
Kimya cha Raila kuhusu Miguna chashangaza wengi

Kimya cha Raila kuhusu Miguna chashangaza wengi

Na BENSON MATHEKA

KINARA wa NASA, Raila Odinga ameshangaza wengi kwa kimya chake kuhusu masaibu ya wakili Miguna Miguna, ambaye alimuapisha kama “rais wa wananchi” Januari 30.

Kimya cha Bw Odinga kimefanya Wakenya na hasa wafuasi wake kutia kwenye mizani mwafaka wake na Rais Uhuru Kenyatta hasa kwa kushindwa kumsaidia Bw Miguna kuingia nchini kutoka Canada.

Japo Odinga alifika katika uwanja wa Kimataifa wa Ndege wa Jomo Kenyatta (JKIA), ambako Bw Miguna alizuiliwa tangu Jumatatu alasiri, hakusema chochote kuhusu hatua ya serikali kumhangaisha.

Bw Miguna alirejea Kenya mnamo Jumatatu, wiki nne baada ya kutimuliwa kwa kumuapisha Bw Odinga kuwa rais wa wananchi, na ilitarajiwa kuwa mwafaka wa wake na Rais Kenyatta ungemsaidia kurejea Kenya na kurudishiwa paspoti yake bila mushkil.

Juhudi za mawakili kushawishi maafisa wa uhamiaji kumruhusu kuingia Kenya hazikufua dafu japo walikuwa na agizo la mahakama.

Bw Odinga alifika katika uwanja huo mwendo wa saa tatu usiku mnamo Jumatatu. Muda mfupi baadaye Bw Miguna alikamatwa machoni pake na maafisa zaidi ya 40 wa polisi waliokuwa na maagizo ya kumwingiza katika ndege ya Emirates iliyokuwa tayari kuelekea Dubai. Bw Odinga hakusema chochote.

“Miguna alinyanyuliwa na maafisa wapatao 40 wa polisi mbele ya Bw Odinga na mawakili wake, kisha akaingizwa katika chumba kilichokuwa chini ya ulinzi mkali kabla ya kulazimishwa kupanda ndege ya kuelekea Dubai. Bw Odinga alitazama tu!” alisema aliyeshuhudia matukio JKIA.

Kiongozi huyo wa chama cha ODM aliondoka uwanja huo punde tu Bw Miguna alipokamatwa bila kuzungumza na wanahabari, tofauti kabisa na ilivyokuwa mfanyabiashara Jimi Wanjigi na mwanamikakati wa NASA David Ndii walipokamatwa.

Hadi wakati wa kuchapisha taarifa hii, Bw Odinga hakuwa ametoa taarifa kuhusu masaibu ya Bw Miguna.

Kufuatia ushirika wake mpya na Rais Kenyatta, wengi walitarajia kuwa angechukua hatua za kumuomba Rais Kenyatta aagize maafisa wa uhamiaji na usalama wa kumruhusu Bw Miguna kuingia nchini na kurejeshewa paspoti yake ili kuepuka kizaazaa kilichoshuhudiwa katika uwanja wa JKIA.

Wadadisi wanasema kwa kukubali kushirikiana na Rais Kenyatta Bw Odinga alijifunga hivi kwamba hawezi kukosoa vitendo dhidi ya washirika wake wa kisiasa.

 

 

You can share this post!

Jaji Kihara na Haji waidhinishwa na kamati ya bunge

Upungufu wa walimu wa Kiswahili wakumba shule za upili

adminleo