• Nairobi
  • Last Updated April 18th, 2024 9:15 PM
Ni kama drama! Miguna akumbana na masaibu zaidi wakati wa Pasaka

Ni kama drama! Miguna akumbana na masaibu zaidi wakati wa Pasaka

Na BENSON MATHEKA

SAKATA ya wakili Miguna Miguna imegeuka kuwa mchezo wa sarakasi ila mchezo wenyewe unahusu masuala mazito ya haki za binadamu na utawala wa kisheria.

Sarakasi hii, ambayo imekuwa ikiendelea filamu ya awamu, maarufu kama series, Alhamisi ilibadilisha mahala pa kuigizia kutoka uwanja wa ndege wa JKIA hadi mjini Dubai, katika msimu huu wa sherehe za Pasaka.

Hii ni baada ya mhusika mkuu, Bw Miguna, kuhamishwa usiku wa manane kutoka chooni ambako alikuwa amezuiliwa kwa takriban saa 48.

Mnamo Jumatano usiku, Bw Miguna alichukuliwa kwa nguvu kutoka chooni uwanjani JKIA, na alipoamka jana alfajiri akagundua hakuwa Nairobi, mbali Dubai katika Muungano wa Milki ya Kiarabu (UAE).

“Nilikuwa nimemuacha ndani ya choo kwenda kumnununua chakula cha jioni kwa sababu hakuwa amekula kwa muda. Niporudi nilipata ameondolewa,” alieleza afisa wa Tume ya Taifa ya Haki za Binadamu (KNHCR), Kamanda Mucheke kwenye ujumbe wa Facebook ambao aliambatanisha na picha zake akiwa na Bw Miguna kwenye choo hicho.

Katika picha nyingine ameshika chakula na kikombe cha chai alizonuia kumpelekea Bw Miguna.

 

Azuiwa kuingia chooni

Bw Mucheke alisema dakika chache baada ya kuondoka Bw Miguna alimpigia simu kumtaka arudi haraka akisema alikuwa kwenye hatari. “Wakati niliporudi, polisi walinizuia kuingia katika choo hicho,” akaeleza Bw Mucheke.

Bw Miguna alikuwa amezuiliwa peke yake katika choo hicho tangu Jumatatu jaribio la kumtimua nchini lilipotibuka alipozua kizaazaa na kushuka ndege ya kwenda Dubai aliyoagizwa kuabiri.

Iliibuka kuwa huenda Bw Miguna alileweshwa dawa hadi akapoteza fahamu kabla ya kubururwa hadi ndege ambayo ilicheleweshwa kwa dakika 28 ikimsubiri.

Mawakili wake Nelson Havi, James Orengo na Julie Soweto walithibitisha kuwa Miguna aliondolewa Kenya wakidai alikuwa ameleweshwa.

Mbunge wa Gatundu aliweka picha kwenye mitandao ya kijamii kuthibitisha wakili huyo alikuwa ndani ya ndege EK722 ya kampuni ya Emirate kuelekea Dubai.

Alhamisi asubuhi, Bw Kuria aliweka video zilizoonyesha Miguna akibishana na maafisa wa usalama katika uwanja wa ndege jijini Dubai.

“Niligutuka nikiwa Dubai na wadhalimu hawa wanasisitiza ni lazima niendelee na safari hadi London. Mimi ni mgonjwa, ninahitaji matibabu. Kuna mmoja anayeitwa Njihia anayenitisha. Ninahitaji msaada haraka. Ninataka kurudi Nairobi. Sitaki kwenda kwingine,” Bw Miguna alieleza kwenye twitter.

 

‘Siogopi kifo’

Kwenye moja ya kanda ambazo Bw Kuria alituma, Bw Miguna anasikika akimwambia mtu aliyevalia sare za wahudumu wa ndege wa kampuni ya Emirates kwamba haogopi kufa na anafahamu sheria za viwanja na uchukuzi wa ndege. “Ukitaka kuniua, fanya hivyo, siogopi kufa, siwezi kutembea,” alisema.

Afisa huyo anasikika akimwambia Bw Miguna kwamba yuko tayari kumtafutia kiti cha magurudumu lakini anakataa.

Kwenye taarifa aliyotuma akiwa Dubai baada ya kusaidiwa na maafisa wa ubalozi wa Canada nchini humo kupata matibabu, Bw Miguna alidai kwamba alivamiwa na zaidi ya maafisa 50 akiwa chooni JKIA.

“Hawakujitambulisha, walinipiga mieleka, wakanifinyilia chini, wakanikalia na wanne miongoni mwao waliweka vitu kwenye mapua yanguhadi nikapoteza fahamu,” alieleza Miguna.

Serikali ya Kenya inasisitiza kuwa Bw Miguna sio raia wa Kenya na anafaa kutoa paspoti ya Canada aliyotumia kusafiri, huku naye akisisitiza arudishiwe paspoti ya Kenya ilivyoagiza mahakama.

Paspoti yake ilitwaliwa na kuharibiwa na serikali alipokamatwa Februari na kutimuliwa Kenya.

Bw Miguna alisema madaktari walithibitisha kwamba alileweshwa na akasema alitarajia kurudi Kenya jana au leo.

 

You can share this post!

Jombi atisha kutimua mke kwa kukataa kuamini ushirikina

Joho amtembelea Miguna hospitalini Dubai

adminleo