• Nairobi
  • Last Updated April 19th, 2024 3:53 PM
Ruto atengwa kuhusu marekebisho ya katiba

Ruto atengwa kuhusu marekebisho ya katiba

Na BERNADINE MUTANU

NAIBU RAIS William Ruto Jumamosi aliendelea kutengwa kwa upinzani wake kwa mapendekezo ya kufanyia marekebisho Katiba iliyopitishwa 2010.

Jumamosi, Muungano wa vyama vya wafanyakazi (COTU-K) ulimwambia Bw Ruto abadili msimamo wake na badala yake awe katika mstari wa mbele kuunga mkono marekebisho kwa lengo la kuhakikisha uwakilishi mpana serikalini.

COTU iliungana na Kanisa Katoliki ambalo Askofu Mkuu Kadinali Njue amesema marekebisho ya Katiba ni muhimu katika kuleta maridhiano ya kitaifa. Muungano wa Makanisa (NCCK) pia umekuwa ukihimiza marekebisho.

Kiongozi wa ANC, Musalia Mudavadi mnamo Ijumaa aliunga mkono marekebisho akisema kuna haja ya kuwa na mfumo wa utawala unaojumuisha wengi.

Wengine ambao wanaunga mkono marekebisho ni kinara wa ODM Raila Odinga ambaye washirika wake wa karibu wametangaza wazi msimamo wao na magavana Alfred Mutua (Machakos) na Wycliffe Oparanya (Kakamega).

Akiongea wakati wa mkutano na wasimamizi wa wafanyikazi, Katibu Mkuu Francis Atwoli alisema muungano huo unataka marekebisho ya Katiba kwa lengo la kuongeza nafasi kuu serikalini.

Alisema marekebisho hayo yanafaa kubuni nafasi ya rais na manaibu kadhaa na waziri mkuu na manaibu wake, kwa lengo la kuzima joto la kisiasa nchini.

“Walete hiyo Katiba turekebishe. Bw Ruto anastahili kujua kuwa anaweza tu kuongoza taifa hili ikiwa kuna amani. Anafaa kuwa katika mstari wa mbele kupigia debe marekebisho ya Katiba,” alisema Bw Atwoli, na kumuonya kuwa ikiwa hataunga mkono azimio hilo, huenda akajipata pabaya.

Wikendi iliyopita, Bw Ruto alipuzilia mbali mjadala kuhusu marekebisho ya Katiba akisema hatua hiyo haifai kwani inalenga kunufaisha watu wachache.

Imeonekana kinaya kwa Bw Ruto kupinga marekebisho ikizingatiwa alikuwa mpinzani mkuu wa Katiba iliyopitishwa 2010, ambapo alikuwa akisisitiza ilikuwa na dosari zilizofaa kurekebishwa kabla ya kuipitisha.

Mapema wiki hii, Bw Ezekiel Njeru aliwasilisha ombi kwa Bunge akihimiza marekebisho. Spika Justin Muturi alisema ombi hilo lilikuwa na uzito uliofaa kutiliwa maanani na akaitaka Kamati ya Sheria kulitathmini na kuwasilisha ripoti katika muda wa siku 60.

 

Kupunguza gharama

Kiongozi huyo wa COTU alisema sababu ya kuunga mkono marekebisho ya Katiba pia ni kupunguza idadi kubwa ya wabunge, ili kupunguza gharama, hasa katika ulipaji wa mishahara na marupurupu, pamoja na kubadilisha sheria za uchaguzi.

“Kenya ni yetu sisi wote, lazima tubadilike jinsi mambo yanavyozidi kubadilika,” alisema Bw Atwoli.

Wakati huo huo, COTU ilimtaka Waziri wa Leba Ukur Yattani “kutopotoshwa” na wanasiasa kuunga mkono mabadiliko ya sheria kuhusu bodi ya Hazina ya Kitaifa ya Malipo ya Uzeeni (NSSF).

“Ikiwa sheria kuhusu itabadilishwa, COTU itaenda mahakamani kutafuta haki, ikiwa mahakama itashindwa kabisa, tuko tayari kuunda hazina yetu ya pensheni,” alisema.

Chama hicho kinapinga mabadiliko yoyote katika hazina hiyo kwa kusema yanalenga kuibua usimamizi mbaya, wizi na uharibifu wa fedha za wafanyakazi.

Pia, muungano huo ulipinga marekebisho ya kifungu cha katiba kinacholinda migomo ya wafanyikazi na mikataba ya mishahara na marupurupu.

Alisema mabadiliko hayo yanahitaji marekebisho ya Katiba kupitia kwa kura ya maamuzi lakini sio kupitia Bungen kama wanavyopendekeza baadhi ya wanasiasa.

Muungano huo uliitaka serikali kutathmini uwezo wa Shirika la Bima la Afya (NHIF) kuchukua kiwango kikubwa cha fedha katika mradi wa bima kwa wanafunzi, kwa kusema huenda shirika hilo likatumiwa kuiba fedha za umma.

Wakati huo, aliitaka serikali kuwaruhusu maafisa wa polisi kuunda chama cha kuwatetea.

You can share this post!

Mfalme wa Swaziland abadili jina la taifa hilo hadi eSwatini

Ruto ajikumbusha maisha ya ‘uhasla’

adminleo