• Nairobi
  • Last Updated March 28th, 2024 9:35 PM
Hospitali 5,000 kuwahudumia wanafunzi kupitia NHIF

Hospitali 5,000 kuwahudumia wanafunzi kupitia NHIF

Na CHARLES WASONGA
SERIKALI imetoa orodha ya hospitali ambazo zitawahudumia wanafunzi wa shule za upili chini ya mpango wa bima ya kitaifa ya matibabu (NHIF).
Zaidi ya shule 8,700 zimepewa orodha ya hospitali 5,314 ambazo kwazo walimu wakuu wanapaswa kuchagua kadhaa na kuwasilisha orodha zao kwa makao makuu ya NHIF. Hospitali hizo zinapatikana kote nchini.
“Mwaombwa kutambua hospitali ambayo zitawahudumia wanafunzi wenu kutoka kwa orodha iliyoandamanishwa na taarifa hii. Hizi ndizo hospitali zilizoidhinishwa… na sharti ziwe karibu na shule husika,” akasema Katibu wa Wizara ya Elimu Belio Kipsang’ katika taarifa kwa walimu wakuu wa shule zote za upili za umma iliyotumwa Aprili 26.
Dkt Kipsang’ aliagiza kila mwalimu mkuu kuwasilisha orodha yake kwa matawi ya NHIF kupitia Wakurugenzi wa Elimu katika kaunti.
Hospitali hizo zitawatambua wanafunzi kwa kutumia data ya wanafunzi zilizohifadhiwa katika Mfumo wa Kitaifa wa Kusimamia Maelezo kuhusu Elimu (NEMIS) huku zikisubiri NHIF kutayatisha kadi maalum za huduma.
Ili kunufaika kwa huduma ya matibabu chini ya bima hiyo mwanafunzi atahitajika kutoa kazi ya uanachama wa NHIF au barua ya kumtambulisha.
“Wanafunzi watawasilisha barua, za kuwatambua zilizoandikwa na walimu wakuu, kwa hospitali hizo.
Barua hiyo sharti iwe na maelezo yafuatayo: Jina la mwanafunzi, Umri/ Jinsia, Jina la Shule, Nambari ya Usajili na sahihi ya shule. Wanafunzi wataanza kufaidi kwa hudumu hiyo mara moja,” kulingana na mwongozo huo.
Dkt Kipsang’ aliwaambia wanahabari kwamba Wizara yake iko tayari kupokea maoni na mapendekezo yoyote ambayo yanaweza kuimarisha mpango huo.
“Tumejitolea kuona kwamba kila mwanafunzi anafaidi. Na wapata huduma za matibabu chini ya mpango huo hata wakiwa likizoni,” akasema Dkt Kipsang’.
Azma kuu ya wizara hiyo ni kuimarisha viwango vya elimu na kuwapunguzia wazazi gharama ya matibabu.

You can share this post!

SHANGAZI: Hasemi nami tena tangu nikatae kumburudisha...

Shujaa yaaga Singapore Sevens kwa alama 10

adminleo