• Nairobi
  • Last Updated March 28th, 2024 11:33 AM
Kaunti za Meru na Embu zapigania miraa

Kaunti za Meru na Embu zapigania miraa

DAVID MUCHUI na CHARLES WANYORO

SERIKALI za Kaunti za Embu na Meru zinazozania Sh2.2 bilioni zilizotolewa kuwafaa wakulima wa miraa katika kaunti hizo.

Huku gavana wa Embu Martin Wambora akisema serikali yake iko tayari kuzungumza na serikali ya Meru kuhusiana na jinsi ya kugawanya pesa hizo, serikali ya Meru imesema kuwa hakuna mazungumzo yoyote ya aina hiyo.

Wambora Jumatano alisema wajumbe kutoka Embu walikuwa katika Kaunti ya Meru kuzungumzia jinsi ya kugawanya pesa hizo na jinsi zitakavyotumiwa.

Alizungumzia Sh1 bilioni, lakini jumla ya Sh2.2 bilioni zilitolewa katika mwaka wa 2016/2017 ambapo Sh1 bilioni zinashikiliwa na Hazina ya Fedha ili kungoja Wizara ya Kilimo kuunda kamati kutekeleza ripoti ya jopo kuhusu miraa iliyotolewa mwaka 2017.

Wambora alisema Embu ililenga kutumia mgao wake kununua miche ya mimea tofauti kwa lengo la kukuza aina tofauti za mazao ili kuepuka kutegemea miraa.

Biashara ya miraa imehusishwa na kiwango kikubwa cha vijana wanaoacha shule eneo hilo.

Alisema uongozi wake ulikuwa umetoa miche 5,000 ya makadamia kwa wakulima katika maeneo wanakopanda miraa.

Hata hivyo, Gavana wa Meru Kiraitu Murungi na chama cha wauzaji miraa cha Nyambene (Nyamita) alipuzilia mbali madai hayo kwa kusema pesa hizo zitatumika kufufua masoko ya miraa.

Bw Kiraitu alisema pesa hizo zitatumika kuambatana na mapendekezo ya jopo kuhusiana na miraa.

“Kwa sasa, Mbunge wa Igembe Kasakazini Maore Maoka ndiye anayefaa kufuatilia suala hilo kwa serikali ya kitaifa kuhusu wakati zitakapotolewa pesa hizo,” alisema.

You can share this post!

ODM kupigania fidia kwa jamii zote zilizopoteza jamaa

Mzozo Knut wachacha huku Sossion akitupwa nje

adminleo