• Nairobi
  • Last Updated April 20th, 2024 7:55 AM
OBARA: Serikali isibadili sembe bila ruhusa ya raia wake

OBARA: Serikali isibadili sembe bila ruhusa ya raia wake

Na VALENTINE OBARA

WIKI iliyopita nilipigwa na butwaa nilopofahamishwa kwamba serikali imenuia kuunda sera ambayo itawalazimu wasagaji mahindi kuchanganya unga huo na ule wa nafaka nyinginezo kama vile mtama, wimbi na mihogo.

Pendekezo hilo lililotangazwa na Katibu wa Wizara ya Kilimo anayesimamia masuala ya mimea na sera, Bw Richard Lesiyampe, linalenga kupunguza jinsi wananchi hula kiwango kikubwa cha mahindi kila mwaka kuliko kile tunachozalisha.

Hakuna ubaya kuchanganya unga wa nafaka hizi kwani hiyo hufanywa na wanaotaka kwa hiari, lakini tatizo lililopo ni kwamba sera hiyo ilivyopendekezwa itaingilia biashara za watu binafsi isivyofaa.

Ulimwenguni kote jukumu la serikali huwa ni kubuni sera ambazo, mbali na kulenga kuboresha maisha ya wananchi wake, hutoa mazingira bora kwa wawekezaji kuendesha biashara zao bila kutatizwa isivyostahili.

Humu nchini inafahamika wazi kwamba unga wa mahindi ni bidhaa muhimu jikoni ndiposa kunapokuwa na uhaba wake, huwa taifa linaingia hofu kwani wengi huhisi kuna janga kuu la ukosefu wa chakula.

Hali huwa hivi hata kama kuna vyakula vingine sokoni kama vile mchele na viazi ambavyo virutubishi vyao vinaweza kuchukua mahala pa mahindi.

Hakika, wawekezaji katika biashara ya kilimo cha mahindi kwenye mashamba makubwa, uagizaji mahindi kutoka mataifa ya nje na utengenezaji wa unga wa mahindi wanafahamu fika jinsi Wakenya wanavyoenzi ugali wa mahindi na hivyo basi faida iliyo katika biashara hii.

Faida ni lengo kuu la biashara yoyote ile, na ni kutokana na faida hii ambapo serikali hupata ushuru wa kutosha kuendeleza majukumu mengine ya kujenga nchi.

Kwa hivyo sera yoyote inayopendekezwa na kupitishwa haifai kudhuru uwezo wa mfanyabiashara kupata faida zake.

Hatari iliyopo kuhusu pendekezo la Bw Lesiyampe ni kwamba linaweza likasababisha hasara kwa waekezaji na athari zake hazitapendeza.

Ingekuwa vyema kama tungeelezwa pendekezo hili lina msingi wake kwa utafiti upi ambao ulipata kuwa Wakenya watajitolea kununua unga wa ugali wenye mchanganyiko wa nafaka.

Kwa mtazamo wangu, hili ni suala ambalo kwanza litahitaji mchango wa wananchi kwani masuala ya unga si ya kufanyiwa mzaha katika nchi hii.

Ni bora serikali iweke mawazo yake na rasilimali kwa juhudi ambazo zinaendelezwa kuongeza kiwango cha mahindi kinachozalishwa kama vile kilimo cha unyunyizaji maji mashambani badala ya kuleta mapendekezo ambayo hayana msingi.

Ilivyo kwa sasa, takwimu zinaonyesha kuwa Kenya huzalisha karibu magunia milioni 40 ya mahindi na kutumia magunia milioni 30 kila mwaka, lakini kuna lengo la kupunguza matumizi hadi milioni 20 ili kusiwe na hatari endapo kutakuwa na mahitaji ya dharura.

Kile ambacho serikali pengine inaweza kufanya kama ina lazima kupunguza matumizi, ni kuweka ushuru kwa unga wa mahindi matupu, na kuondoa ushuru kwa bidhaa nyingine zinazoweza kuchukua mahala pa unga wa mahindi ikiwemo unga huo wa mchanganyiko ambao unaweza kuleta hasara kwa biashara.

 

You can share this post!

Aliyefanyiwa upasuaji vibaya akijifungua Gatundu afariki

Kipa Oluoch aikosesha Gor ushindi ugenini Rwanda

adminleo